Serikali imewaeleza mabalozi njia mbalimbali inazozitumia kudhibiti maambukizi ya virusi vya corona ikiwa ni pamoja na kuridhia uingizwaji wa chanjo ya Uviko 19 kwa Balozi, Taasisi na Mashirika ya Kimataifa yanayotaka kufanya hivyo.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula (Mb) amewaeleza baadhi ya Mabalozi wanaotoka katika nchi za Kiislamu wakati alipokutana nao kwa ajili ya kuhitimisha sherehe za Eid El Haj leo jijini Dar es Salaam.

Pia Balozi Mulamula amefafanua kuhusiana na maswali aliyokuwa akiulizwa na baadhi ya mbalozi juu ya chanjo ya kukabiliana na ugonjwa wa Uviko 19 na kusema kuwa hakuna Balozi, Taasisi au Mashirika ya Kimataifa yalizuiliwa kuingiza chanjo kwaajili ya kuwachanja watu wao na kuwasihi kutoa taarifa kwa wizara ya Afya ili kuwezesha namna bora ya kuratibu na kupokea chanjo hizo.

“…….Naomba niwahakikishie waheshimiwa mabalozi kuwa Serikali yetu ni sikivu sana, nimekuwa nikiulizwa maswali mbalimbali kuhusu uingizwaji wa chanjo kwa ajili ya kuwachanja watumishi katika balozi zenu hapa nchini ila naomba msisite kuwasiliana na Wizara ya Afya kwa ajili ya kuratibu njia bora ya kupata chanjo hiyo,” Amesema Balozi Mulamula.

Katika tukio jingine, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula amekutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Canada nchini Mhe. Pamela O’Donnell pamoja na Balozi wa Uingereza nchini Mhe. David Concar.

Balozi Mulamula amekutana na mabalozi hao kwa nyakati tofauti katika Ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam ambapo awali amekutana na Balozi wa Canada nchini, Mhe. Pamela O’Donnell akifuatiwa na Balozi wa Uingereza nchini Mhe. David Concar kwa lengo la kujadiliana masuala mbalimbali ya uhusiano wa kidiplomasia baina ya Tanzania na nchi zao.

Pamoja na mambo mengine, viongozi hao wamejadili masuala mbalimbali ya kuendeleza na kuimarisha ushirikiano wa uwili (Bilateral Cooperation).

Waziri Ummy aitembelea Coastal Union kambini
TTCL yatakiwa kuonesha ushindani