Shughuli za Mahakama zimekwama nchini Uganda kufuatia mgomo wa waendesha mashtaka wakidai nyongeza mishahara na marupurupu ambayo wamekuwa wakilalamikia Serikali kwa muda mrefu bila kusikilizwa.

Mbali na kutaka kuboreshewa mazingira salama ya kazi, wasimamizi hao wa mashtaka wanataka kiwango cha mishahara kipandishwe kutoka shilingi 644,000 za Uganda mpaka hadi shilingi milioni 9, huku mkuu wa mashtaka akitaka kupokea mshahara wa miioni 40, kutoka shilingi milioni 10 anazopokea kwa sasa.

Aidha, msemaji wa mahakama wa nchi hiyo, Solomon Muyita amesema kuwa waendesha mashtaka hao 300 wanataka kuongezwa idadi yao pia kuongezewa marupu rupu yao kwa asilimia 40.

“Tumelazimika kusitisha shughuli za mahakama, Majaji hawawezi kufanya kazi bila wasimamizi wa mashtaka Idara ya mahakama imeathirika pakubwa na mgomo huu, hakuna mtuhumiwa yeyote atakayeachiliwa kwa dhamana hadi mgomo utakapomalizika,”amesema Muyita.

Kwa upande wake Mwendesha Mashtaka  Mkuu ya umma nchini humo,  Mike chibita amesema kuwa ataitisha mkutano utakao washirikisha wahusika wote ili kujadili baadhi ya mambo ambayo yamesababisha mgomo huo.

Hata hivyo, Serikali, kupitia kwa Waziri Mkuu Dkt. Ruhakana Rugunda, amesema kuwa Waziri wa Haki na Katiba, Jenerali Kahinda Otafire anashughulikia swala hilo, bila kutoa maelezo zaidi.

 

 

Ambwene Yessaya (AY) amvisha pete Remy
Trump ajitathmini, aanza kulegeza misimamo yake