Klabu ya Soka ya Simba imefanikiwa kuibuka na ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya Mwadui FC, katika mchezo wa ligi kuu Tanzania bara uliofanyika kwenye uwanja wa taifa jijini Dar es salaam.

Simba sasa imefikisha alama 36 na kupanda kutoka nafasi ya 5 hadi nafasi ya tatu kwenye msimamo wa ligi ikizishusha timu za Lipuli FC yenye alama 36 ikizidiwa wastani wa mabao ya kufunga na kufungwa pamoja na KMC yenye alama 35.

Mchezo huo kwa Simba ni wa 15 huku kwa Mwadui FC ukiwa ni mchezo wa 25 hivyo Simba ina takribani viporo vya mechi 10 kwenye ligi, mechi ambazo zimetokana na ushiriki wao kwenye ligi ya mabingwa Afrika ambapo wapo hatua ya makundi.

Kwa upande wa msemaji wa Simba, Haji Manara amesema kuwa walizihitaji sana pointi tatu za mchezo huo na wamefanikiwa kuzipata.

”Tulizihitaji pointi tatu tunashukuru tumezipata, hongereni wachezaji na benchi lote la ufundi sambamba na mashabiki wetu, sasa tunawangoja Mafarao,”amesema Manara

Hata hivyo, baada ya mchezo wa Simba na Al Ahly Jumanne ijayo, Simba itakipiga na klabu ya Yanga kwenye pambano la watani wa jadi siku ya Jumamosi Februari 16, 2019

LIVE BUNGENI: Yanayojiri Bungeni jijini Dodoma
Habari kubwa katika magazeti ya Tanzania leo Februari 8, 2019