Simba SC imefufua matumaini ya kwenda Robo Fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika baada ya ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Al Ahly kwenye mchezo wa Kundi D uliochezwa katika Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.
 
Bao pekee katika mchezo huo, limefungwa na mshambuliaji wa kimataifa wa Rwanda, Meddie Kagere dakika ya 65 kwa shuti kali baada ya kupokea pasi ya kichwa kutoka kwa nahodha na mshambuliaji wa kimataifa wa Tanzania, John Raphael Bocco kufuatia krosi ya beki Zana Coulibaly kutoka Burkina Faso.
 
Kwa ushindi huo, Simba SC inafikisha pointi sita baada ya kucheza mechi nne ikipanda kwa nafasi moja hadi ya pili, nyuma ya Al Ahly wenye pointi saba mbele ya AS Vita ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) yenye pointi nne na JS Saoura ya Algeria yenye pointi mbili.
 
Aidha, Simba SC watahamishia makali yao kwenye Ligi Kuu ya Tanzania Bara ambapo wanatarajia kumenyana na watani wao wa jadi, Yanga SC Jumamosi kabla ya kusafiri kuwafuata JS Saoura Machi 9 kabla ya kurejea nyumbani kumalizia na AS Vita Machi 16.
 
Hata hivyo, timu mbili za juu zitaungana na washindi wengine wa makundi A, B na C kwenda Robo Fainali ya michuano hiyo.
 
Kikosi cha Simba SC kilikuwa; Aishi Manula, Zana Coulibally, Asante Kwasi/Mohammed Hussein ‘Tshabalala’ dk39, Juuko Murshid, Serge Wawa, James Kotei/Muzamil Yassin dk90+2, Jonas Mkude, Clatous Chama, John Bocco/Hassan Dilunga dk82, Emmanuel Okwi na Meddie Kagere.
 
  • Simba yaanza kuvitafuna viporo vyake, ‘Sasa tunawasubiri Mafarao
 
  • Simba yaongeza nguvu Ligi ya Mabingwa Barani Afrika
 
  • Simba yaufyata kwa AS Vita, yapokea kipigo cha ‘Mbwa koko’
 
Al Ahly: Mohamed El Shenawy, Ayman Ashraf, Ali Maaloul, Yasser Ibrahim, Mohamed Hany, Amr Al Sulaya, Ramadan Sobhi, Karim Nedved/ Salah Mohsen dk84, Hussein El Shahat, Hamdi Fathi/ Nasser Maher dk70 na Oluwafemi Junior Ajayi

CCM Njombe waeleza siri ya mafanikio mbele ya viongozi wa Kitaifa
Wakulima na Wafugaji waliopata majanga waanza kunufaika