Kikosi cha Wekundu wa Msimbazi, Simba SC kimeondoka alfajiri ya leo jijini Dar es Salaam kuelekea mkoani Shinyanga kwaajili ya mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya Mwadui FC ya mkoani humo.

Mchezo huo utafanyika Alhamisi wiki hii katika dimba la Mwadui Complex.

Simba ambao ndiyo vinara wa ligi hiyo, inakwenda kupambana na Mwadui ikiwa imetoka kuipa kichapo Timu ya Gendermarie ya Djibout mabao 4-0 katika michuano ya Kombe la Shirikisho barani Afrika mchezo uliopigwa Jumapili iliyopita katika dimba la Taifa Dar es Salaam.

Kuelekea mechi hiyo, msemaji wa Simba Haji Manara amesema wataingia kwenye mchezo huo kwa tahadhari kubwa kutokana na wapinzani wao kuwa kwenye kiwango kizuri kwasasa ikitoka kuichapa Mtibwa Sugar mabao 3-1 katika dimba hilo.

Manara amesema ushindani katika ligi unazidi kuongezeka, na timu yoyote inaweza kufikia idadi ya pointi walizonazo hivyo hawawezi kuidharau Timu ya Mwadui licha ya kuwazidi pointi 23 katika msimamo wa ligi, Simba ikiwa na pointi 41 huku Mwadui wakiwa na pointi 18 katika nafasi ya 13.

Nyoka adaiwa kumeza mamilioni ya fedha
Ligi ya Mabingwa Ulaya kuendelea leo