Simba SC imepoteza mechi ya kwanza Kundi D Ligi ya Mabingwa Afrika baada ya kuchapwa mabao 5-0 na wenyeji, AS Vita Uwanja wa Martyrs de la Pentecote zamani Kamanyola, uliopo eneo la Lingwala jijini Kinshasa, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC).

Kipigo hicho kinakuja baada ya Simba SC kuanza vyema mchezo wake wa kwanza ikishinda 3-0 dhidi ya JS Saoura ya Algeria Jumamosi ya wiki iliyopita jijini Dar es Salaam na kuwapa matumaini Watanzania kwamba inafanya vizuri.

Kundi D linaongozwa na Al Ahly wakiwa na pointi zao nne, wakifuatiwa AS Vita pointi tatu sawa na Simba huku JS Saoura ikishika mkia kwa pointi yake moja.

Mshambuliaji Jean-Marc Makusu Mundele ndiye aliyeanza kuwianua mashabiki wa AS Vita baada ya kufunga bao la kwanza dakika ya 14 akimalizia pasi ya Glody Ngonda Muzinga

Beki Botuli Padou Bompunga aliyekuwa anacheza badala ya Dharles Kalonji ambaye anatumikia adhabu ya kadi nyekundu, aliifungia AS Vita bao la pili dakika ya 19 akimalizia kona ya Ngonda.

Aidha, haikuishia hapo tu, kalamu ya magoli iliendelea baada ya kiungo, Fabrice Luamba Ngoma akiifungia AS Vita bao la tatu kwa penalti dakika ya 45 akimtungua kipa namba moja wa Tanzania, Aishi Salum Manula kufuatia beki wa Simba SC, Pascal Wawa kumuangusha mchezaji huyo kwenye boksi.

Kocha wa Simba alianza kipindi cha pili kwa kufanya mabadiliko katika safu ya kiungo, akimtoa Muzamil Yassin na kumuingiza Mnyarwanda, Haruna Niyonzima kabla ya kumtoa Mzambia, Clatous Chama na kumuingiza Hassan Dilunga.

Hata hivyo, mabadiliko hayo hayakuzaa matunda kwa Simba baada ya beki, Makwekwe Kupa kufunga bao la nne kwa kichwa dakika ya 71 akimalizia kona nzuri iliyochongwa na Tuisila Kisinda, kabla ya Makusu kuwachambua mabeki wa Simba na kipa wao, Manula kuifungia Vita bao la tano dakika ya 74 kufuatia pasi nzuri ya Kazadi Kasengu.

Kikosi cha Simba SC kinatarajia kugeuza leo kurejea jijini Dar es Salaam kucheza michuano ya SportPesa Super Cup kabla ya kusafiri kwenda kumenyana na Al Ahly.

Video: Mayweather atinga kwenye chumba cha Pacquiao, kuzichapa?
Mahakama yahalalisha matokeo ya DRC, mpinzani ang’aka