Serikali ya Somalia imemfukuza nchini humo Balozi wa Umoja wa Mataifa, Nickolas Haysom kwa madai kuwa ameingilia mambo ya ndani ya nchi hiyo.

Taarifa ya kumfukuza Haysom imemtaka kuondoka mara moja na kwamba hatakiwi tena kurejea ndani ya nchi hiyo akidaiwa kuhoji masuala ambayo ni ya ndani ya nchi yanayoleta sintofahamu.

Haymon aliandika barua yenye maswali kadhaa kwa Serikali, akiitaka kutoa maelezo kuhusu kuuawa kwa watu waliokuwa wanaandamana kupinga kukamatwa kwa kiongozi wa zamani wa Al Shabaab, Sheikh Muktari Roobow mjini Baidoa, Desemba 13 mwaka jana.

Balozi huyo alitaka kufahamu kuhusu hatua na nguvu iliyotumika na kusababisha kuuawa kwa watu 15 katika mvutano wa kumkamata kiongozi huyo.

Barua hiyo iliyoelekezwa kwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya nchi hiyo, ilitaka kufahamu kuhusu ushiriki wa wanajeshi ambao wanaungwa mkono na Umoja wa Mataifa katika kukamatwa kwa Roobow. Alifafanua kuwa, kwa mujibu wa taratibu na mikataba ya kimataifa, usaidizi wa majeshi ya Umoja wa Mataifa hutumika katika kulinda haki za binadamu na sio vinginevyo.

Sintofahamu hiyo imesababisha Umoja wa Ulaya kusitisha misaada yake kwa jeshi la polisi la Somalia.

Wakati mzozo huo ukiendelea, wanamgambo wa al Shabaab walishambulia ngome kambi ya jeshi la Umoja wa Somalia kwa kurusha makombora saba ndani ya kambi hiyo, lakini kwa mujibu wa umoja huo hakuna watu waliopata majeraha mabaya.

“Shambulizi la leo la makombora kwenye kambi ya Umoja wa Mataifa ni ukiukwaji wa sheria za kimataifa za binadamu. Ninalaani kitendo hiki kisichokuwa na sababu yoyote dhidi ya wafanyakazi wetu,” imeeleza barua ya Haysom.

Kambi iliyoshambuliwa inatajwa kuwa ni kambi kubwa zaidi ya Umoja wa Mataifa iliyo na wanajeshi wa nchi mbalimbali, inayofahamika kama ‘Halane Center’.

Fid Q asaliti kambi ya makapera, ajimilikisha rasmi jiko
Rais Magufuli awageukia watumishi... 'msiseme maagizo kutoka juu'