Wizara ya Afya imekabidhi vifaa kwa ajili ya huduma ya tiba mtandao kwenye hospitali ya Rufaa ya Mkoa-Songea.

Akizungumza wakati wa makabidhiano hayo Mratibu wa huduma za Tiba Mtandao kutoka Wizara ya Afya Dkt. Liggyle Vumilia amesema kuwa vifaa hivyo ni awamu ya pili ili kukamilisha mfumo mzima wa huduma hizo ambapo vitasaidia upatikanaji wa huduma za afya za kibingwa na ubingwa bobezi bila kujali umbali wa mteja alipo.

Dkt. Liggyle ameongeza kuwa watoa huduma wa hospitali hiyo watapata majibu sahihi na kwa wakati ili kuweza kutoa matibabu kwa wagonjwa wao kwani mfumo huo unaunganishwa na vifaa na mashine za kidigitali (CT-Scan, Digital X-Ray, Utra sound scan) zilizofungwa na zitakazofungwa kwenye hospitali hiyo pamoja na kuunganishwa na hospitali za rufaa za Kanda, Maalumu na Taifa.

“Mtoa huduma atatuma picha kwa hospitali yeyote yenye kuhitaji utaalamu wa juu zaidi kwenda hospitali za Kanda na Kitaifa kulingana na tatizo la mgonjwa, hivyo huduma hii itapungza gharama za matibabu,usafiri kwa wananchi walio pembezoni mwa nchi ambapo awali walikua wakizifuata MOI, JKCI au Muhimbili” na pia kupunguza tatizo la kutokuwa na wataalamu mabingwa kwenye hospitali za pembezoni.

Aidha, Dkt. Liggyle amesema Serikali imetoa vifaa hivyo katika hospitali ya rufaa ya mkoa Bombo, Tanga na Katavi na kuongeza kuwa lengo ni kuzifikia hospitali za rufaa za mikoa 21 hapa nchini.

Awali akipokea vifaa hivyo Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa-Songea Dkt.Magafu Majura ameishukuru Wizara ya Afya kwa kuwapatia vifaa hivyo ambavyo vitawasaidia wananchi katika huduma za kibingwa na bobezi pamoja na kuwapunguzia gharama za usafiri wa kufuata vipimo nje ya mkoa, vilevile nchi za jirani za Malawi na Msumbiji.

Vifaa hivyo vya Tiba Mtandao vimefadhiliwa na Mfuko wa Mawasiliano kwa wote(UCSAF)

Zimbabwe na Tanzania kujengeana Uwezo wa Madini
Wakandarasi wababaishaji kupigwa buti na Serikali