Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Job Ndugai amempiga kijembe mbunge wa Iringa, Peter Msigwa kwa kumwambia anaumia kumuona mbunge mpya wa CCM, Joseph Mkundi wa jimbo la Ukerewe mkoani Mwanza akichangia bungeni.

Ameyasema hayo bungeni jijini Dodoma kwenye kipindi cha maswali na majibu ambapo alimkaribisha kuuliza swali mbunge huyo aliyeapishwa leo Novemba 15, 2018.

“Karibu Mheshimiwa mbunge mpya kabisa wa Chama Cha Mapinduzi kupitia Jimbo la Ukerewe Joseph Mkundi, namuona mheshimiwa Msigwa inamuuma sana”, amesema Ndugai.

Aidha, mbunge huyo wa Ukerewe, Joseph Mkundi ameapishwa leo Bungeni, baada ya kupita bila kupingwa katika uchaguzi mdogo wa Ubunge uliofanyika hivi karibuni kufuatia mbunge huyo kujiuzulu nafasi yake akiwa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) na kuhamia CCM kisha kugombea tena.

Katika swali lake alihoji ni lini serikali itapeleka gari la wagonjwa katika kituo cha afya cha Bwisya, ambacho kilitumika kuhudumia wahanga wa ajali ya MV Nyerere mapema mwezi Agosti.

Akijibu swali hilo, Waziri wa Afya, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu amesema kuwa serikali itanunua magari ya wagonjwa 70 na moja litapelekwa katika kituo hicho cha Afya kama ilivyoelekezwa na Rais Dkt. Magufuli

Tanzania yanyimwa msaada wa dola mil. 9 kisa kuzuia Ushoga
Uingereza yaidhinisha rasimu ya kujitenga na Umoja wa Ulaya