Wakati dirisha la usajili wa wachezaji watakaoshiriki ligi kuu ya soka Tanzania bara na ligi daraja la kwanza likifunguliwa rasmi hii leo, chama cha wachezaji wa soka nchini SPUTANZA, kimetoa angalizo kwa viongozi wa klabu na wachezaji.

Mwenyekiti wa SPUTANZA Mussa Kisoki amesema kuna haja kwa kila mchezaji kujitathmini na kujitambua kabla ya kufanya maamuzi ya kusaini mkataba na klabu yoyote kwa sasa, ili kuepuka matatizo ambayo huenda yakawaingiza kwenye kifungo cha kushindwa kucheza soka kwa mwaka mmoja ama zaidi.

Kisoki amesema kabla ya dirisha la usajili kufunguliwa rasmi leo, SPUTANZA imekua ikiona na kusoma katika vyombo vya habari, taarifa za baadhi ya wachezaji kusaini mikataba na klabu za ligi kuu, jambo ambalo amesema lina umuhimu kwa pande zote mbili, lakini akasisitiza suala umakini.

Amesema kila mchezaji mwenye kutambua na kukumbuka mkataba wake wa klabu aliyoituimikia msimu uliopita unakwisha lini, atakua na uhuru wa kufanya hivyo, lakini kwa wale ambao wanakosa kumbukumbu ni bora wakajiridhisha, kabla ya kufanya maamuzi ya kusaini mkataba na klabu mpya.

“Kuna haja kwa kila mchezaji kuangalia suala hili ambalo ni muhimu sana katika kipindi hiki, lengo letu ni kuwaisaidia wachezaji ili waweze kucheza soka kama sehemu ya ajira yao.

“Hatupendi kuona wanakaa bila kucheza, maana watakua wanakosa kipato na kujishushia viwango vya vya uchezaji wao, binafsi ninawaomba sana wawe makini katika kipindi hiki ambacho kina umuhimu katika maisha yao.” Amesema Kisoki.

Hata hivyo Mussa Kisoki amewataka viongozi wa klabu za ligi kuu na madaja ya chini kuheshimu mikataba ya wachezaji na klabu walizozitumikia msimu uliopita, ili wasiwaingize kwenye matatizo ambayo huenda yakawagharimu.

Makamu wa Rais mgeni rasmi mchezo wa Everton na Gor Mahia, aipongeza SportPesa
Roma Mkatoliki Arudi Shule ya Msingi, Aongeza Nguvu Kwenye Hisabati