Aliyekuwa kocha mkuu wa timu ya taifa ya Nigeria, Sunday Oliseh ameipongeza timu ya taifa ya Ufaransa kwa kutwaa ubingwa wa dunia kwa mara ya pili baada ya miaka 20.

Oliseh ambaye alikuwa mchezaji wa Nigeria wakati wa Fainali za Kombe la Dunia za 1998 ambazo zilishuhudia Ufarsana wakitwaa ubingwa wa dunia kwa mara ya kwanza, amesema hana budi kuipongeza timu hiyo kutokana na uwezo na uwajibikaji mkubwa waliouonyesha tangu walipoanza kampeni ya kusaka mafanikio huko Urusi.

Oliseh amesema kwa upande mwingine anaamini Ufaransa imekuwa timu ya kwanza duniani kuiwakilisha vyema Afrika, kutokana na kuwa na wachezaji wengi kutoka bara hilo.

Amesema hali hiyo inadhihirisha Afrika kuna uwezo mkubwa kisoka na kuna kila sababu ya mataifa ya bara hilo kuthamini na kuendeleza vipaji vya wachezaji wao, ili kufuata nyayo za wachezaji wa Ufaransa ambao wengi wao wa asili ya Afrika.

“Wakati mwingine ninajivunia timu hii na kuamini Afrika imetwaa ubingwa kupitia taifa la Ufaransa, imenifunza mambo mengi sana, hasa ukiangalia namna mataifa ya Afrika yalivyojaa wachezaji wenye uwezo mkubwa kisoka,”

“Tunapaswa kuiga mfano mzuri kutoka kwa Ufaransa, waliwaona na kuwathamini wachezaji hawa licha ya kuwa na asili ya Afrika, lakini waliamini wanaweza kulitangaza vyema taifa lao, na leo (Jana) wameweza kufanikisha malengo yao.”

“Hakuna kinacho shindikana chini ya jua, kila taifa la Afrika likijipanga na kutambua mchango wa wachezaji wenye uchungu wa kucheza kwa kujituma wakati wote, ipo siku tutafanikisha lengo, kama ilivyo kwa Ufaransa ambao waliamua kutumia fursa ya wachezaji wenye asili yetu.”

“Bado ninasisitiza kwa maono yangu mimi ninasema Afria imetwaa ubigwa kwa mara ya kwanza kupitia taifa la Ufaransa,” amesema Oliseh ambaye alikua mkuu wa benchi la ufundi la Nigeria kuanzia mwaka 2015–2016.

Akiwa kama mchezaji Oliseh aliitumikia Nigeria kuanzia mwaka 1993–2002.

Katika fainali za kombe la dunia mwaka huu 2018 Afrika iliwakilishwa na mataifa ya Nigeria, Misri (Egypt), Senegal, Tunisia na Morocco lakini timu zote hizo zilitolewa kwenye hatua ya makundi.

Video: CCM itatawala milele, wanaohangaika watapata tabu sana - JPM
Hukumu ya Wema yasogezwa mbele