Idadi kubwa ya maduka makubwa ya bidhaa (Supermarkets) yametii agizo la Mamlaka ya Chakula na Dawa Tanzania (TFDA) la kuzuia uingizaji nyama kutoka Afrika kusini.

Hatua hiyo imekuja baada ya soseji zinazotengenezwa huko aina ya Polony kubainika kuwa na ugonjwa wa listeriosis ulioasababisha vifo vya watu 180 nchini humo.

Soseji hizo zinatengenezwa na kiwanda cha Tiger Brand Unit Enterprises na cha RC Foods vya Afrika Kusini.

Katika taarifa yake Machi 7, TFDA ilisema usitishaji utaendelea hadi hapo itakapothibitishwa kuwa bidhaa hizo ni salama .

Hata hivyo msemaji wa TFDA, Gaudencia Simwanza amesema bado wanaendelea kufanya uchunguzi kubaini kama bado kuna maduka yanayouza soseji na nyama za kusaga.

”Tunaendelea na kazi ya ukaguzi ndani na mipakani kuona kama bidhaa hizo bado zinaingizwa nchini tutakachobaini tutawafahamisha”. amesema Gaudencia.

Ugonjwa wa Listerious ni aina ya bakteria ambao hupatikana kwenye maji, ubongo na kinyesi , na binadamu huambukizwa pale wanapotumia vyakula au maji yenye bakteria hao.

Visababishi vikubwa vya bakteria Listeriosis ni nyama na maziwa mabichi.

Aidha madaktari wameeleza kuwa bakteria hao ni hatari sana na wanaweza kusababisha kifo kwani hushambulia mfumo wa fahamu wa damu.

Mlipuko wa Listeriosis ulianza Disemba mwaka jana na mpaka sasa umesababisha vifo vya watu 180 huko Afrika kusini.

Sisafiri kwenda nje kwa sababu sio jimbo langu- Rais Dkt. Magufuli
JPM: Sitishwi wala sitishiki, niko kwa ajili ya Watanzania