Imeelezwa kuwa tafiti mbalimbali zinazofanywa na wataalam katika eneo la kilimo cha umwagiliaji zinasaidia katika kupatikana kwa suluhu na kutatua changamoto za uwekezaji katika sekta hiyo.

Hayo yamesemwa jijini Dar es salaam na Kaimu Mkurugenzi waTume ya Taifa ya Umwagiliaji Mhandisi Dkt. Eliakimu Chitutu alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari.

Amesema kuwa tafiti hizo zinaweza kusaidia kuishauri Serikali katika kusimamia miundombinu ya kilimo cha umwagiliaji na matumizi bora ya maji kwa wakulima.

“Skimu nyingi zinatumia njia za asili kama mifereji na sisi tunahamasisha wakulima kutumia teknolojia za kisasa katika kilimo cha umwagiliaji kama vile kilimo cha matone yaani Drip irrigation.”Amesema Chitutu.

Aidha, ameongeza kuwa kwasasa Tume ya Umwagililiaji inafanya tafiti mbalimbali katika mikoa ya Dodoma, Iringa na Morogro kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo kama vile Shirika la tafiti kutoka Japan ambalo linalenga katika kuangalia tija ya maji katika skimu ya umwagiliaji.

Akizungumzia Mipango ya Tume ya Taifa ya Umwagiliaji, Mhandisi Chitutu amesema kuwa Tume imekuwa ikiendelea na ujenzi wa skimu za Umwagiliaji kadri ambavyo pesa zimekuwa zikipatikana na imeweza kufanya upembuzi yakinifu, ukarabati, maboresho na upanuzi wa skimu nyingi za umwagiliaji nchini.

Hata hivyo, Mhandisi Chitutu ameongeza kuwa Tanzania ina eneo lenye ukubwa wa Hekta Milioni 29.4 zinazofaa kwa kilimo cha umwagiliaji ambapo kati ya hizo, hekta milioni 2.3 zina uwezo wa juu wa kumwagiliwa na hekta milioni 4.8 zina uwezo wa kati ambapo hekta milioni 22.3 ndizo zimendelezwa mpaka June 2018.

 

Majaliwa awahakikishia wanakijiji kupata huduma safi ya maji
Makonda amjibu Dudu baya sakata la mashoga