Taharuki imezuka leo asubuhi ndani ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania baada ya kusikika mlio wa tahadhari (alarm) mara mbili kwa nyakati tofauti.

Mlio huo uliwafanya baadhi ya wabunge kushindwa kuvumilia na kutoka nje wakiwa wanakimbia.

Mwenyekii wa Kikao cha Bunge, Najma Giga alitangaza kusitisha kikao hicho cha Bunge kufuatia sintofahamu hiyo.

Imeelezwa kuwa mlio wa tahadhari (alarm) ulisikika majira ya saa tano na dakika mbili, hadi saa tano na dakika nane.

Lakini, mlio huo wa tahadhari ulisikika kwa mara ya pili baada ya dakika 10 tangu usikike mlio wa kwanza, hivyo kumlazimu Mwenyekiti kuchukua uamuzi wa kusitisha kikao hicho.

Mbunge wa Muleba Kaskazini, Charles Mwijage akikimbia kutoka nje ya Bunge baada ya mlio wa hatari kusikika (Picha kwa hisani ya Mwananchi)

Kamanda wa Polisi mkoa wa Dodoma, Gilles Muroto alifika bungeni hapo  na aliwaambia waandishi wa habari kuwa ni mapema kueleza chanzo cha mlio huo. Alisema tayari jeshi hilo kwa kushirikiana na Kikosi cha Zimamoto na Uokoaji wanaendelea na kazi ya kubaini chanzo na kutafuta ufumbuzi.

Mwanamke aliyepotea baada ya kukodi Taxi akutwa amekufa
Mawaziri kulipwa mishahara na marupurupu maisha yao yote