Timu ya soka ya Tanzania ‘Taifa Stars’, kesho Septemba 3, 2016 inatarajiwa kuingia kibaruani kwa kucheza na Super Eagles ya Nigeria katika mchezo wa mwisho wa hatua ya makundi kuwania nafasi ya kucheza fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON 2017).

Mchezo huo utafanyika kuanzia saa 11.00 (17h00) jioni kwenye Uwanja wa Kimataifa wa Godswill Akpabo, mjini Uyo katika Jimbo la Akwa Ibom. Muda huo uko mbele kwa saa mbili kamili kwa maana hiyo Taifa Stars itacheza dhidi ya Nigeria saa 9.00 alasiri (15h00).

Taifa Stars iliyoondoka Dar es Salaam, Tanzania jana alfajiri, na wachezaji 18 kabla ya kuungana na Nahodha wa timu hiyo, Mbwana Samatta nchini Nigeria, ilitua salama mjini Uyo ambako imefikia Hoteli ya Le Meridien Ibom & Golf Resort. Samatta – Mshambuliaji wa kimataifa wa Tanzania anayechezea timu ya Genk ya Ubelgiji ya jijini Brussels.

Licha ya mchezo huo kuwa sehemu ya mchuano wa kuwania nafasi ya kucheza fainali hizo za AFCON 2017 huko Gabon, lakini utakuwa ni wa kukamilisha ratiba baada ya Misri kufuzu kwa fainali hizo kutoka kundi G ambalo mbali ya Nigeria na Tanzania, pia ilikuwako Chad ambayo iliyojitoa katikati ya mashindano.

Mwisho Wa Kujisajili GPX Ni Jumatatu
Ligi Kuu Tanzania Bara Kuendelea Kesho