Wapenzi na mashabiki wa Simba SC wameanza kuingiwa na hofu kufuatia mfanyabiashara maarufu Mohamed Dewji kutoa taarifa ya kuharakisha mchakato wa kutaka kuinunua klabu hiyo yenye maskani yake mtaa wa Msimbazi jijini Dar es salaam.

Tajiri huyo maarufu kama MO, mara kadhaa amekuwa akinukuliwa na vyombo mbalimbali vya habari akielezea nia yake ya kutaka kuwekeza kwenye klabu hiyo ili iondokane na umasikini

Lakini katika hali ya kutatanisha, jana Disemba 29 alitoa taarifa kwa baadhi ya vyombo vya habari akidai kwamba ametoa siku tatu kwa viongozi wa Simba kumpa majibu ya adhma yake hiyo, vinginevyo atafuta mpango wake.

Maana yake ni kwamba hadi kufika kesho Disemba 31 endapo Simba itakuwa kimya, hatoendelea tena na mpango huo.

Kupitia mitandao mbalimbali ya kijamii, wapenzi na wadau mbalimbali wa Simba SC wameonyesha wasiwasi mkubwa kwamba pengine kuharakisha huko kunaweza kusiwe na nia njema.

Wapo wadau waliokuwa wanashauri kuwepo kwa muda wa kutosha wa kushughulikia suala hilo na si kama anavyoshinikiza MO.

Mijadala hiyo ilionekana kushika hatamu tangu usiku wa Jumanne Disemba 29 hadi alfajiri ya Disemba 30.

Mohamed Dewji anadai kufanya majadiliano na viongozi hao kwa zaidi ya miezi miwili, amechoka na kutopewa majibu ya kueleweka, kwani hadi sasa amekutana na Rais wa Simba Evans Aveva na viongozi wengine ila hakuna majibu.

Hivyo uamuzi wake ni kuwa katoa siku tatu kuanzia Disemba 29 hadi 31, 2015 viongozi watoe jibu la kukubali au kukataa.

Kama utakuwa unakumbuka vizuri Mohamed Dewji ‘MO’ ambaye anataka kuinunua Simba kuiendesha kibiashara kwa kuwekeza bilioni 20 za kitanzania, mwezi Machi 2015, alitajwa na jarida la Forbes la Marekani kuwa moja kati ya mabilionea 29 wa Afrika akiwa nafasi ya 24 kwa kuwa na utajiri wa dola bilioni 1.3 ambazo ni sawa na Tsh trilioni 2.34

Bamford Aubomoa Mkataba Wa Crystal Palace
Leicester City Wabanana Na Manchester City