Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) mkoani Rukwa imeokoa Sh. 170 Milioni zilizokuwa zimeibwa na watu wasio waaminifu kupitia vikundi mbalimbali vya kuweka akiba.

Mkuu wa Takukuru Mkoa wa Rukwa, Hamza Mwenda ametoa taarifa hiyo alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusu kazi iliyofanywa na Taasisi hiyo kati ya Aprili na Juni, 2020.

Mwenda amesema kuwa watuhumiwa ni viongozi wa kata na vijiji waliokuwa wamepewa kazi na Halmashauri zao kukusanya mapato kupitia mfumo wa POS (Point of Sales Machine).

Kati ya fedha zilizookolewa, Sh. 59 Milioni zilipaswa kuwa malipo kwa walimu wastaafu 39 waliokuwa wanachama wa Saccos ya CHAUWAMI Wilaya za Kalambo na Sumbawanga.

Alifafanua kuwa, ingawa wazee hao walistaafu miaka minne iliyopita, viongozi wa CHAUWAMI Saccos hawakuwalipa fedha zao na hawakuonesha nia ya kuwalipa hata wakati huu.

Taasisi hiyo ilibaini kuwa viongozi wa Saccos hiyo walikuwa wanaweka fedha za michango kwenye akaunti zao binafsi, kinyume cha Sheria.

Katika hatua nyingine, Takukuru ilikabidhi kiasi cha Sh. 39 Milioni kwa viongozi wa Saccos ya walimu ya Nkasi baada ya kubaini kuwa viongozi wanaomaliza muda wao wanajaribu kufanya ubadhirifu. Pia, ilibainika kuwa viongozi hao waliokuwa wamemaliza muda wao walikuwa wanagushi nyaraka na kuwakopesha watu ambao sio wanachama wa Saccos hiyo, kinyume cha taratibu.

Mkuu huyo wa Takukuru Rukwa alibainisha kuwa walifanikiwa kuokoa kiasi cha Sh. 34.2 Milioni zilizoibwa na watu wasio waaminifu waliokuwa wanatumia POS kukusanya mapato.

“Watu hao walifanya makusanyo, lakini badala ya kuweka fedha hizo kwenye akaunti za benki za Halmashauri, waliziweka mifukoni mwao,” amesema.

Ameongeza kuwa katika kipindi hicho, Taasisi hiyo pia iliokoa Sh. 45 Milioni, ilizozidishiwa kampuni ya Girson Investment Ltd, iliyofanya kazi ya kujenga bwawa la kumwagilizia lililopo katika Kata ya Kirando, Wilaya ya Nkasi.

Gavana Kenya apinga ripoti ya Wizara, adai hakuna Covid-19 kwake

Kenya yanyoosha maelezo kuhusu Watanzania kuingia kwao

Mtoto mdukuzi sugu wa Twitter ashikishwa adabu, alimdukua Obama, Bill Gates
Video: Maneno ya Diamond kwa mume wa Esma