Siku chache baada ya Wananchi wa vijiji vya Nyamande, Kitandililo na Ibatu Kata ya Kitandililo Halmashauri ya mji wa Makambako mkoani Njombe, kuiomba Serikali kupitia kwa viongozi wa chama cha mapinduzi (CCM) kufikisha huduma ya Umeme katika vijiji hivyo hatimaye ombi hilo limeanza kutafutiwa ufumbuzi.

Wananchi hao waliwasilisha ombi hilo kwa Katibu wa Siasa na Uenezi (CCM) mkoa humo, Erasto Ngole alipotembelea vijiji vya kata hiyo baada ya kuzungumza na wananchi, aliipokea changamoto hiyo ya ukosefu wa huduma ya umeme na kuahidi kuifanyia kazi.

Katibu huyo wa CCM mkoa wa Njombe ameifikisha katika Ofisi ya TANESCO mkoani humo kwa kukutana na Meneja wa Ofisi hiyo Muhandisi, Suleman Mghwira, kisha kuzungumza naye ambaye amekiri uwepo wa changamoto hiyo katika Vijiji mbalimbali ndani ya mkoa wa Njombe na kuahidi kutafuta ufumbuzi.

Kwa upande wake meneja huyo amesema kuwa Vijiji vya Nyamande, Kitandililo na Ibatu vimeanza kufikishiwa huduma ya umeme kupitia wakala wa nishati vijijini REA awamu ya tatu, tayari nguzo za umeme zimeshaanza kusimikwa katika vijiji hivyo sambamba na kuahidi kumsimamia mkandarasi ili akamilishe kazi hiyo kwa haraka.

“Tunatambua uwepo wa changamoto ya huduma ya umeme katika baadhi ya vijiji vya kata ya Kitandililo ikiwemo shule ya Sekondari Kitandililo na kata nyingine katika mkoa wetu wa Njombe, nitahakikisha mkandarasi huyu anakamilisha kazi kwa wakati, pia kuna tatizo kama hili katika vijiji vya Itulike kata ya Ramadhani, Jumapili nitafika Mtaa wa Itulike ili kuzungumza na wananchi,”amesema Mghwira

Hata hivyo Meneja huyo wa Tanesco ameahidi kushirikiana na Viongozi mbalimbali wa chama na Serikali pamoja na wananchi, ili kutatua tatizo hilo huku akiahidi kufika katika Kijiji cha Itulike kata ya Ramadhani mjini Njombe, kuzungumza na wananchi juu ya tatizo la umeme kijijini hapo na kutafuta ufumbuzi.

Muongozaji wa filamu John Singleton afariki Dunia
Sababu yatajwa wanaume wengi kukosa nguvu za kiume