Katibu Mkuu Mstaafu Ofisi ya Waziri Mkuu, Mussa Uledi amesema kuwa Tanzania inanufaika kiuchumi kama mwanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika
(SADC) pamoja na jumuiya nyingine ambazo Tanzania ni mwanachama.

Ameyasema hayo mjini Morogoro wakati akiwasilisha mada ikiwa ni siku ya pili ya mafunzo kwa waandishi wa habari ya kuwajengea uwezo wa kuandika na kuripoti habari za SADC, ambapo amesema kuwa nchi yetu imenufaika na utekelezaji wa miradi ya miundombinu, biashara, uwekezaji na viwanda.

“Mkakati wa maendeleo wa SADC unafafanana kwa kiwango kikubwa na ule wa Tanzania ambao pia unazingatia haja ya utekelezaji wa viwanda na miundombinu hapa nchini, hali itakayochangia katika kuimarisha maendeleo na kukuza uchumi na ustawi wa wananchi,”amesema Uledi

Aidha, amesema kuwa vipaumbele vya Tanzania vimejikita katika upanuzi wa Mauzo nje na uongezaji wa michepuo yake, lengo likiwa ni kukuza na kuendeleza biashara hali inayowezesha uendelezaji wa viwanda vya kuongeza thamani katika malighafi za ndani hususani mazao ya kilimo na madini.

Hata hivyo, Uledi ameongeza kuwa ziara ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt’ John Pombe Magufuli katika baadhi ya nchi wanachama wa SADC imeonyesha kuwa Tanzania imejipanga vizuri kimkakati inaweza kuwa ghala la Chakula kwa kukuza zaidi uzalishaji kuendana na mahitaji katika soko la jumuiya hiyo na hata nje ya jumuiya.

 

Mbunge atoa angalizo uuzaji wa Mahindi mkoani Njombe
ICC yamkuta na hatia ya mauaji, ubakaji aliyekuwa Mkuu wa Majeshi