Tasnia ya habari nchini imepata pigo kwa kumpoteza mtangazaji maarufu wa kituo cha redio cha E-FM, Seth Katende maarufu kama ‘Bikira wa kisukuma’ aliyefariki leo mchana katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili.

Taarifa za kifo cha mtangazaji huyo aliyekuwa akisikika kupitia kipindi cha ‘Ubaoni’ zimethibitishwa na uongozi wa E-FM. Kituo hicho cha redio kimeeleza kuwa Katende alipoteza maisha baada ya kuugua kwa muda mfupi.

“Kwa masikitiko makubwa E FM inapenda kuwajulisha kuwa mwenzetu Seth Katende maarufu” Bikira wa kisukuma”amefariki dunia Leo mchana katika hospitali ya Taifa ya Muhimbili baada ya kuugua kwa muda mfupi.Seth atakumbukwa sana kwa ucheshi wake kupitia kipindi cha Ubaoni alichokua akiendesha sambamba na Imma Kapanga na Mpoki au “mwarabu wa Dubai”.Msiba upo nyumbani kwa baba yake mzazi Changanyikeni Dar es salaam,” imeeleza taarifa ya E-FM.

Katende alianza kupata umaarufu kupitia mtandao wa Instagram akitumia jina la ‘Bikira wa Kisukuma’ akichambua mada mbalimbali za maisha zilizowagusa wengi hususan vijana.

Umaarufu wa marehemu uliongezeka mara dufu baada ya kuanza kusikika kupitia kipindi cha Ubaoni cha E-FM kutokana na ucheshi wake na jinsi alivyokuwa akiwasilisha mada mbalimbali.

Dar24 imeguswa na msiba huu na kwa masikitiko makubwa uongozi na wafanyakazi kwa pamoja wanatoa pole kwa familia, ndugu, jamaa na marafiki wa marehemu pamoja na Watanzania wote kwa ujumla. Mungu ampumzishe kwa amani. Amina!

Video: Kama uliikosa hii, Banana Zorro alivyomvuta Saida Karoli jukwaani akiimba "Mpenzi Nakupenda"
Video: Majaliwa awahakikishia wawekezaji mafanikio