Tasnia ya habari na burudani imepata pigo kwa kuondokewa na Mkurugenzi wa Uzalishaji na Vipindi wa Clouds Media Group, Ruge Mutahaba.

Taarifa ya kufariki kwa gwiji huyo mwenye mchango mkubwa zimetolewa jioni hii, ambapo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Magufuli ametuma salamu zake za rambirambi kupitia mtandao wa Twitter.

“Nimepokea kwa masikitiko taarifa za kifo cha kijana wangu Ruge Mutahaba. Daima nitamkumbuka kwa mchango wake mkubwa ktka tasnia ya habari, burudani na juhudi za kujenga fikra za maendeleo kwa vijana. Poleni wana familia, ndugu, jamaa na marafiki. Mungu amuweke mahali pema, Amina,” ametweet Rais Magufuli.

Ruge amefariki akiwa hospitalini nchini Afrika Kusini alikokuwa akipatiwa matibabu.

Kwa mujibu wa taarifa zilizotolewa na familia yake, alikuwa akisumbuliwa na tatizo la figo.

Dar24 tumeguswa na msiba huu, na tunawapa pole Watanzania wote, ndugu jamaa na familia ya Ruge Mutahaba. Mungu ampumzishe kwa amani. Amina!

Habari kubwa katika magazeti ya Tanzania leo Februari 27, 2019
NMB yatumia zaidi ya bil.1 kusaidia mashule