WAKALA wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA), umeendelea kurejesha mawasiliano katika maeneo mbalimballi yaliyoathiriwa na mvua nchini na kusababisha adha kwa watumiaji wa barabara hizo pamoja na madaraja.

Kwa Mikoa ya Dodoma na Manyara, tayari mawasiliano yanaendelea kurejeshwa kwa halmashauri ya wilaya ya Babati, halmashauri ya wilaya ya Mbulu, halmashauri ya wilaya ya Babati Mji na halmashauri ya wilaya ya Kondoa.

Meneja wa wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini TARURA katika halmashauri ya wilaya ya Babati mhandisi Said Mikongomi ameeleza kuwa tayari wamerejesha mawasiliano katika maeneo mbalimbali na sasa wananchi wanaendelea na shughuli zao za kiuchumi.

‘‘Tumeanza kurejesha mawasiliano katika maeneo mbalimbali ili wananchi waweze kupita na kuendelea na shughuli zao za kiuchumi, maeneo yaliyorekebishwa ni Pamoja na daraja la Masware ambalo tayari linapitika na daraja hili pia linapitisha malighafi zinazoenda katika kiwanda cha sukari cha Babati’’

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu Hudson Kamoga ameeleza kuwa maeneo yaliyoharibiwa na mvua tayari yanapitika na kuongeza kuwa kazi zinazofanywa na TARURA zimeleta mageuzi makubwa kwa wananchi kwani wataalamu wa wanafika mapema sana pale changamoto inapotokea.

Katika halmashauri ya wilaya ya Kondoa mkoani Dodoma, mawasiliano pia yamerejeshwa ambapo daraja la Kalamba tayari limefanyiwa matengenezo na wananchi wanavuka bila shida.

Meneja wa TARURA katika halmashauri ya wilaya ya Kondoa mhandisi Goodluck Mbanga ameeleza kuwa mvua zilizonyesha zilikata mawasiliano katika Daraja la Kalamba lakini hadi sasa tayari matengenezo yamefanyika na wananchi wanasafiri bila shida huku akifafanua kuwa matengenezo makubwa yataendelea kufanyika kwa mwaka wa fedha ujao.

Oxfam kufunga ofisi zake nchi 18 Tanzania yatajwa
Michezo kurudi Juni Mosi