Kamati ya Utendaji ya Chama cha Waandishi wa Habari za Michezo Tanzania (TASWA) ilikutana Dar es Salaam Mei 24, 2016 kujadili masuala mbalimbali.

A; Tuzo za Wanamichezo Bora

Kikao kilikubaliana Tuzo za Wanamichezo Bora zinazotolewa kila mwaka na TASWA, safari hii zifanyike Agosti 26, mwaka huu, Dar es Salaam zikihusisha michezo mbalimbali.

TASWA imeuanda kamati maalum kwa ajili ya kusimamia upatikanaji wa wanamichezo hao bora, kamati ambayo inajumuisha waandishi waandamizi kutoka vyombo mbalimbali vya habari na wataalamu kutoka vyama mbalimbali vya michezo. Sekretarieti ya TASWA inaendelea kufanya mawasiliano na wateule wa kamati hiyo kabla ya kuwatangaza.

Kwa kawaida kila mwaka TASWA inatoa tuzo kwa wanamichezo bora wa kila mchezo na pia kunakuwa na mwanamichezo bora wa jumla kwa mwaka husika.

Baadhi ya waliopata kutwaa tuzo ya Mwanamichezo Bora Tanzania wa jumla kwa miaka kumi iliyopia na miaka yao katika mabano ni Samson Ramadhani (2006), Martin Sulle (2007) na Mary Naali (2008) wote wanariadha.

Mwaka 2009 tuzo ilienda kwa mcheza netiboli Mwanaidi Hassan, ambaye pia alitwaa tuzo hiyo mwaka 2010, wakati mwaka 2011, ambapo tuzo yake ilitolewa mwaka 2012 mshindi alikuwa mwanasoka Shomari Kapombe. Mwaka 2013/2014 ilienda kwa mwanasoka Sheridah Boniface.

Mwaka 2015 tuzo ilifanyika katika aina nyingine,  ambapo walizawadiwa wanamichezo 10 tu waliofanya vizuri zaidi katika miaka 10 ya urais wa Jakaya Kikwete na pia TASWA ilitoa Tuzo ya Heshima kwa Kikwete.

B; Media Day

Kama inavyojulikana chama chetu kimekuwa kikiandaa bonanza maalum likihusisha waandishi na wafanyakazi wa vyombo mbalimbali vya habari hapa nchini, lakini kwa miaka miwili bonanza hilo limekwama kufanyika kutokana na sababu mbalimbali. Kikao kimekubaliana nguvu zaidi ielekezwe ili jambo hilo lifanyike na kuwapa raha wadau. Taarifa zaidi kuhusu Media Day itatolewa Jumamosi wiki hii.

C: Changamoto kwa waandishi

Kikao kilijadili changamoto mbalimbali zinazowakabili waandishi wa habari za michezo na chama kwa ujumla, ambazo zimewekewa mikakati ya muda mfupi na mrefu na utekelezaji wake utaanza kuonekana siku chache zijazo.

Ahsanteni,

Amir Mhando

Katibu Mkuu TASWA

Video: Jambo hili lisipo pata majibu leo Mh. Waziri nakwambia hapahapa nakufa na wewe - Doto Biteko
Audio: Jay – Z airukia ‘All the Way Up’ ya Fat Joe na Remy Ma