Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), imewataja wamiliki wa Wasafi TV ambapo jina la Joseph Kusaga, mmiliki wa Clouds Media Group halikutajwa kama baadhi ya watu walivyokuwa wanafikiria.

Kupitia tangazo lake lililosambaa jana la nia ya kuipa leseni Wasafi TV, ambalo lilimtaka mtu yeyote mwenye pingamizi au maoni kuwasilisha katika Mamlaka hiyo ndani ya siku 14, limewataja watu watatu wenye hisa katika uwekezaji huo.

“Maoni ya maandishi yanakaribishwa kutoka kwa mtu aliyeguswa kutolewa leseni kwa mwombaji na yaifikie Mamlaka ndani ya siku 14 tangu kuchapishwa kwa tangazo hili,” imeeleza taarifa hiyo ya TCRA.

Waliotajwa ni Juhayna Zaghalulu Ajmy ambaye anamiliki asilimia 53 ya hisa, Nasibu Abdul Juma (Diamond) anayemiliki asilimia 43 ya hisa na Ali Khatib Dai anayemiliki asilimia 2.

Hata hivyo, Juhayna Zaghalulu Ajmy ambaye ndiye mwenye hisa nyingi zaidi anatajwa kuwa na uhusiano wa karibu na Clouds Media Group akiwa ni mke wa Joseph Kusaga.

Pia, anatajwa kuwa mmoja wa wamiliki wa kampuni ya Primetime Promotions ambao ni washirika wakuu wa Clouds Media Group.

Wasafi TV tayari imeanza kurusha matangazo yake katika hatua za majaribio na inaelekea kuanza kazi rasmi endapo leseni hiyo itatolewa.

Diamond na timu ya Wasafi imekuwa kwenye mgogoro mkubwa na timu ya Clouds Media Group katika kipindi cha hivi karibuni, mgogoro uliochochewa zaidi na matamasha yao ya Fiesta na Wasafi Festival.

Gianluca Vialli: Nipo Vizuri japo siijui kesho yangu
Habari kubwa katika magazeti ya Tanzania leo Novemba 27, 2018