Zaidi ya watu 380 wamethibitishwa kufariki kufuatia tetemeko la ardhi lililoambatana na tsunami lililoikumba Indonesia jana.  

Tetemeko hilo lililosababisha mawimbi yenye urefu hadi wa mita 3, lilifagia eneo la kisiwa cha Sulawesi.

Kipande cha video cha tukio hilo kinaonesha watu wakipiga kelele kuomba msaada huku majengo ikiwa ni pamoja na msikiti yakiharibiwa vibaya.

Taharuki kubwa imeendelea kuikumba nchi hiyo. Maelfu ya makazi ya watu yameharibiwa kabisa pamoja na sehemu za huduma za kijamii kama hospitali, hoteli na maduka makubwa.

Wakala wa kudhibiti majanga nchini Indonesia imeeleza kuwa hadi sasa watu waliopoteza maisha ni 384 lakini idadi hiyo inatarajiwa kuongezeka. Imeeleza pia kuwa zaidi ya watu 540 wamejeruhiwa.

“Miili mingi imekutwa pembezoni mwa bahari kutokana na tsunami, lakini idadi yao kamili itatajwa hapo baadaye,” msemaji wa Wakala wa kudhibiti majanga, Sutopo Purwo Nugroho aliiambia Reuters.

“Wakati hatari hii inatokea jana, watu walikuwa bado wanaendelea na shughuli zao za uvuvi ufukweni na hawakuweza kukimbia haraka, wengi wamekuwa wahanga,” aliongeza

Alisema watu walionusurika wakiwa ufukweni ni wale tu ambao walifanikiwa kupanda miti yenye urfu wa mita sita kukwepa mawimbi.

'Nahodha wa MV Nyerere hakuwa na vigezo'
Rais Magufuli: Sipendi kutumbua, tena siku hizi sipendi hata kulisikia hilo neno