Shirikisho la Mpira wa Miguu Nchini Tanzania (TFF) limeishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na wadau wa soka nchini walioiunga mkono timu ya Taifa, ‘Taifa Stars’ wakati wa maandalizi ya mchezo wa kwanza wa kufuzu fainali za kombe la Dunia 2022 dhidi ya Burundi.

Hayo yameelezwa na TFF kupitia taarifa ambayo imetolewa leo na shirikisho hilo huku ikiishukuru wizara ya mambo ya nje, ubalozi, wizara ya michezo, waandishi wa habari pamoja na Watanzania waliosafiri hadi Burundi kwa ajili ya kuishangilia Taifa Stars dhidi ya timu ya taifa hilo.

Aidha, katika mchezo huo uliopigwa nchini Burundi ulimalizika kwa sare ya bao 1-1 ambapo mabao hayo yaliyofungwa kipindi cha pili cha mchezo huo ambapo bao la Burundi lilifungwa na Cedric Amisi kwenye dakika ya 81 huku vijana wa Kitanzania wakisawazisha kupitia Simon Msuva katika dakika ya 85.

Taifa Stars inatarajiwa kuwasili leo majira ya saa 11: 35 jioni kwa usafiri wa ndege ya Air Tanzania.

Mchezo wa marudiano utapigwa nchini Tanzania Septemba 8, 2019 siku ya jumapili katika uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam ambapo TFF imetoa rai kwa Watanzania na wadau wa soka kujitokeza kwa wingi siku ya jumapili kuiumga mkono Taifa Stars.

Nigeria yatuma ndege nne Afrika Kusini
Mbowe ang'aka Bungeni, 'Hii si sawa kwa kanuni hizi'