Kampuni ya simu za mkononi wa Tigo ambayo ni mdhamini mkuu wa tamasha la Fiesta mwaka huu lililobatizwa jina la ‘Tigo Fiesta’ linaloandaliwa na Clouds Media Group, imedaiwa kuwazuia Mwana FA na AY kushiriki tamasha hilo.

Kwa mujibu wa wasanii hao, kampuni hiyo sio tu kwamba imewazuia kutumbuiza bali pia wamezuiwa kuhudhuria kwenye tamasha hilo kama mashabiki na nyimbo zao zimepigwa marufuku.

Mkali huyo wa ‘Dume Suruali’ ameripotiwa kuzuiwa getini alipojaribu kuingia kwenye tamasha hilo lililofanyika jana jijini Arusha ambapo alienda kama shabiki wa kawaida.

FA ametoa ujumbe huo akiwa ameuweka katika hali ya kejeli na mshangao akihoji uhalali wa marufuku ya kampuni hiyo ambayo walisigana nayo mahakamani hivi karibuni wakiidai zaidi ya shilingi bilioni 2 na kuishinda.


Kwa upande wa AY, alikumbushia zuio la nyimbo zao kupigwa kwenye tamasha hilo ambalo lilidhaminiwa pia na Tigo.

Hivi karibuni, Mahakama Kuu ilibariki uamuzi wa Mahakama ya Wilaya wa kuitaka kampuni hiyo kuwalipa AY na FA kiasi cha zaidi ya shilingi bilioni 2 baada ya kujiridhisha kuwa walitumia nyimbo zao mbili kama miito ya simu bila idhini yao. Kesi hiyo ilidumu kwa takribani miaka mitano.

Mwanasheria wa wasanii hao, Alberto Msando amesema kuwa kitendo cha kuwazuia wasanii hao kuingia kwenye tamasha hilo ni cha kitoto na cha ajabu.

Magazeti ya Tanzania leo Septemba 11, 2017
Video: Makonda azindua kiwanda cha wajasiliamali