Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imewataka wananchi kuchukua tahadhari kuelekea katika kipindi cha msimu wa mvua za masika, Machi hadi Mei 2020.

Akizungumza jana na waandishi wa habari, Mkurugenzi Mkuu wa TMA, Dkt. Agnes Kijazi alisema kuwa mikoa inayotarajia kupata mvua za kawaida na zaidi ni Tanga, Unguja, Arusha, Manyara, Kilimanjaro, Geita, Mwanza, Shinyanga, Simiyu na Kisiwa cha Pemba.

“Kipindi kifupi cha mvua kubwa kinatarajiwa kuathiri hata maeneo ambayo yalikuwa yanategemea kupata mvua za kawaida au hata mvua zilizo chini ya kiwango cha kawaida, hivyo ni muhimu kuchukua hatua za tahadhari ili kuepuka madhara hasi zaidi,” alisema Dkt. Kijazi.

Alitaja maeneo ambayo yanatarajia kupata mvua za kawaida kuwa ni pamoja na Dar es Salaam, Pwani na maeneo ya Mafia. Pia, alitataja maeneo ya Kaskazini mwa Morogoro kuwa sehemu ya maeneo hayo.

Hivi karibuni, Dar24 Media kupitia kipindi cha ‘On The Bench’ iliwakutanisha wataalam kutoka TMA na Mipango Miji, pamoja na wananchi wanaokaa katika maeneo ya Jangwani jijini Dar es Salaam, eneo ambalo kwa kiasi kikubwa huathirika na mvua.

Wananchi hao walitoa sababu za kuendelea kuhatarisha maisha yao katika maeneo hayo wakiamini kuwa mvua huwa na msimu na zikiisha wanaendelea na maisha, walishauriwa kuhama na kuelezwa hatari inayoweza kuwakumba.

 

Yemen: Watu 31 wauawa shambulizi la anga
Mtoto wa miaka 12 ajiua baada ya kutuhumiwa kuiba Sh 6,000