Hatimae fununu za uongozi wa klabu ya Man Utd za kutaka kuvunja mkataba wa meneja wa klabu ya Tottenham, Mauricio Pochettino na kisha kumtangaza kama mbadala wa Louis Van Gaal, zimeingia gizani, baada ya uongozi wa Spurs kumsainisha mkataba mpya.

Pochettino, ambaye msimu huu ameonyesha maajabu ya kuifikisha Spurs katika uwezo wa kuwania ubingwa wa nchini England kabla ya kuzidiwa kete na Leicester City huku michezo mitatu ya mwishoni mwa msimu ikisalia, alikua akitajwa sana katika vyombo vya habari kuhusu safari ya kuelekea kukinoa kikosi cha Man Utd.

Muda mchache uliopita uongozi wa Spurs, umethibitisha kumalizana na meneja huyo kutoka nchini Argentina na mkataba wake mpya unampa nafasi ya kuwepo White Hart Lane hadi mwaka 2021.

 Mauricio Pochettino akiwa katika picha ya pamoja na mwenyekiti wa Spurs, Daniel Levy sambamba na safu yake ya benchi la ufundi, baada ya kukamilisha hatua ya kusaini mkataba mpya.

Safu ya benchi la ufundi ambayo ipo chini ya Pochettino, nayo imesainishwa mkataba mpya, ikiwa ni sehemu ya kuimarisha mikakati ya kufanya vizuri zaidi msimu ujao wa ligi.

Safu ya benchi la ufundi la Spurs iliyosainishwa mikataba mipya ni Jesus Perez, Miguel D’Agostino pamoja na Toni Jimenez.

Everton Wamtimua Roberto Martinez
Young Africans Watangaza Watakavyofanya Sherehe Za Ubingwa