Klabu ya Tottenham Hotspurs imewaomba radhi mashabiki wake, kufuatia mpango wa kurejea kwenye uwanja wao wa White Hart Lane Oktoba 29 wakati wa mchezo ligi ya England dhidi ya mabingwa watetezi Manchester City kwenda mrama.

Taarifa iliyotolewa na mwenyekiti wa klabu hiyo ya jijini London Daniel Levy imeeleza kuwa, mpango wa kurejea uwanjani hapo utachelewa kutokana na kampuni ya ukandarasi waliyoingi nayo mkataba kuendelea kufanya matengenezo ya hatua za mwisho.

Levy amesema mchezo huo wa ligi utachezwa kwenye uwanja wa Wembley wanaoutumia tangu msimu uliopita kama uwanja wao wa nyumbani.

Kiongozi huyo pia amethibitisha michezo mitatu ya ligi ya mabingwa barani Ulaya dhidi ya FC Barcelona (Oktoba 03), PSV Eindhoven (Oktoba 06) na Inter Milan (Novemba 28) itachezwa kwenye uwanja wa Wembley.

“Tunajitahidi kukamilisha matengenezo kwa muda tulioukusudia, changamoto ndogondogo zimekua kikwazo na tumeona kuna haja ya kuendelea kucheza michezo yetu kwenye uwanja wa Wembley,”

“Tunafahamu mashabiki wana hamu ya kurejea katika uwanja wao, na niwahakikishie muda utafika na tutarejea katika sehemu yetu tulioizoea ambayo itakua na muonekano mpya.” Alisema Daniel Levy

Spurs walikua wamepanga kurejea katika uwanja wao rasmi wakati wa mchezo wa ligi dhidi ya Liverpool Septemba 15, lakini changamoto zilizojitokeza zimeendelea kuwa kikwazo cha kuanza kuutumia uwanja huo, uliopo kaskazini mwa jijini London.

LIVE: Yanayojiri Bungeni Dodoma Leo Septemba 4, 2018
Video: Wanaohama Chadema wanasumbuliwa na njaa, CCM ni wezi tu- Doita