Wahandisi wazalendo wametakiwa kujipanga ili kuweza kuchangamkia fursa za uwekezaji katika miradi mbalimbali ya bandari nchini.

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi Mkuu wa TPA, Mhandisi Deusdedit Kakoko wakati akizungumza katika warsha iliyoandaliwa na Chama cha Wataalamu, Washauri wa Wahandisi ‘ARINI Association of Consulting Engineers Tanzania’, (ACET).

Amesema kuwa malengo ya TPA kwenye warsha hiyo ni kuwafahamisha uwepo wa miradi mikubwa ya maendeleo, hivyo wanatakiwa kuchukua nafasi hiyo ili kuendeleza bandari kwa huduma zao kupitia miradi iliyopo na kuwaasa wachangamkie fursa zilizopo.

“Bandarini kuna fursa ya kazi za ujenzi wa miundombinu katika nyanja zote kama ujenzi wa mitambo, umeme, mafuta, gesi na TEHAMA,” amesema Mhandisi Kakoko.

Amesisitiza kuwa changamoto kubwa kwa sasa ni pamoja na kutochukua hatua za makusudi za kuchangamkia fursa kwa makampuni ya ujenzi ya ndani, uwezo mdogo wa makampuni ya wahandisi, wataalam wachache wenye weledi pamoja na vikundi vya taaluma kutoshirikiana.

Aidha, amesema kuwa kuna haja ya kutoa taarifa za ufuatiliaji na maeneo ya changamoto mpya mara kwa mara na kwa pamoja ili kupata ufumbuzi wa haraka.

Kwa upande wake Rais wa ACET, Mhandisi Mpembe Ngwisa amesema kuwa TPA imefanya tukio kubwa na la kihistoria kundaa warsha kama hiyo kwa wahandisi.

Naye Kaimu Mkurugenzi wa Mipango ya Miundombinu na Uwekezaji, wa TPA, Mhandisi Allen Banda amesema kwamba miradi yao mingi imefanikiwa kwa sababu ya uwepo wa wahandisi washauri.

 

Makonda amvutia kasi Amber Rutty, amtaka ajisalimishe polisi
UVCCM kuajiri vijana 300, wadai BAVICHA sio saizi yao