Shirika la Reli Tanzania (TRC) limefanikiwa kufufua reli inayounganisha Tanzania na Jiji la Kampala nchini Uganda, ambayo ilikufa kwa kipindi cha miaka kumi, ambayo imekuza kiwango cha biashara kati ya nchi hizo mbili kufikia asilimia 5.5 kutoka asilimia 1 ya awali.

Hayo yamesemwa Jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Reli nchini (TRC), Masanja Kadogosa, ambapo amesema kuwa katika kipindi cha miaka miatatu, Shirika hilo limefanya maboresho kadhaa yaliyoongeza ufanisi wa utendaji kazi katika uendeshaji wa reli nchini.

“Njia ya reli kwenda Kampala tuliyoifufua hivi karibuni baada ya kutotumika kwa miaka 10, imesadia kukuza biashara ya kusafirisha mizigo kutoka asilimia 1.5 hadi 5.5, na pia imeweza kupunguza muda wa safari kutoka siku nane hadi kufikia siku nne,” Amesema Kadogosa

Ameongeza kuwa maboresho hayo yaliyofanyika katika kipindi cha miaka mitatu yamesaidia kuongezeka kwa kiwango cha mizigo kinachosafirishwa kutoka tani 150 hadi 180 na kufikia tani 100,002  katika kipindi cha robo ya kwanza ya mwaka, ambayo ni sawa na asilimia 60.

Aidha, ametaja maboresho mengine yaliyofanyika kuwa ni kufungua stesheni mbalimbali kama ya Tanga, pamoja na kuongeza njia za kupishana treni, pia kutandika upya njia ya treni kutoka Dar es Salaam hadi Pugu yenye urefu wa km 20, sambamba na kuboresha njia ya Ubungo ambayo imeongeza makusanyo kutoka shilingi milioni 1 hadi  shilingi milioni 6.5.

Hata hivyo, Mkurugenzi huyo wa TRC, amebainisha kuwa shirika hilo lina mradi wa kuboresha reli ya kati yenye urefu wa km 2600, ambapo amesema ni njia muhimu inayoounganisha nchi kwasasa, pamoja na kutumika kusafirishia vifaa vya ujenzi wa reli mpya ya kisasa yaani Standard Gauge.

 

Vijana, Wanawake na Walemavu waneemeka Sumbawanga
FA awaombea msamaha WCB, Basata wampa masharti