Rais wa Marekani Donald Trump amesaini sheria mpya ya kuongeza vikwazo dhidi ya Korea Kaskazini kutokana na mpango wake wa nyuklia, Trump pia amesema kuwa benki kuu nchini China imeagiza benki nyingine za China kuacha kufanya biashara na Korea Kaskazini.

Tayari waziri wa fedha wa Marekani ameidhinisha vikwazo hivyo dhidi ya makampuni ya fedha yanayofanya biashara zake ndani ya Korea Kaskazini.

Hatua hii inakuja katika kipindi cha chini ya wiki mbili baada ya umoja wa mataifa kuidhinisha vikwazo vipya dhidi ya taifa hilo kwasababu ya jaribilo lake la hivi karibuni la nyuklia.

Wakati hayo yakiendelea rais wa Korea Kaskazini Kim Jong-un amemuita Tramp mropokaji asiyefikiria na kwamba kauli anazotoa Trump zinamfanya ajione yuko sahihi kuendelea na mipango yake ya nyuklia.

Katika taarifa isiyo ya kawaida kupitia vyombo vya habari vya serikali kiongozi wa Korea Kaskazini alisema Trump atajutia hotuba yake ya hivi karibuni aliyoiotoa kwa Umoja wa Mataifa.

Hali ya wasi wasi imetanda katika kipindi cha wiki za hivi karibuni kutokana na hatua ya Korea Kaskazini kufanya majaribio ya makombora ya masafa marefu, licha ya shinikizo kutoka kwa mataifa tajiri zaidi duniani kuitaka iachane na majaribio hayo.

 

 

Makala: Soko la biashara miaka hii ni gumu kulinganisha na miaka ya nyuma.
Msigwa: Tuko tayari kuuza kila kitu chetu kugharamia matibabu ya Lissu