Rungu la serikali kufungia kampuni 27 za utangazaji limevipiga pia vituo vinavyomilikiwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM), Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Mwanza, Anthony Diallo pamoja na Robert Lowassa ambaye ni mtoto wa aliyekuwa mgombea urais kupitia Chadema, Edward Lowassa.

Vituo hivyo vimefungiwa kutokana na kufanya kosa la kutolipa ada na tozo mbalimbali zilizowekwa kwa mujibu wa sheria.

Hayo yamebainika baada ya kutajwa kwa orodha ya makampuni hayo yaliyofungiwa na Mamlaka ya Mawasiliano nchini (TCRA). Meneja Mawasiliano wa TCRA, Innocent Mungy alisema kuwa vituo hivyo vimefungiwa kwa kipindi cha miezi mitatu kuanzia Januari 18 hadi Aprili 17 mwaka huu.

“Ni makosa makubwa kwa kampuni ya utangazaji kutolipa ada na tozo na hatua tulizochokua ni za awali endapo kampuni itashindwa kulipa deni hilo kwa kipindi cha miezi mitatu, hatua zaidi zitachukuliwa ikiwa ni pamoja na kulipa faini au kufutiwa leseni au vyote kwa pamoja,” Mungy anakaririwa.

Vituo hivyo ni Radio Uhuru Fm iliyoko jijini Dar es Salaam inayomilikiwa na CCM, Radio Five Fm iliyoko jijini Arusha liyomilikiwa na Robert Lowassa ambaye ni mtoto wa Edward Lowassa.

Tangazo la kuifungia Star Tv ilizua mjadala kutokana mchango wake mkubwa kwa Chama Cha Mapinduzi wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu pamoja na ahadi ya Rais John Magufuli wakati wa kampeni kuwa angemlinda mmiliki wa kituo hicho, Anthony Diallo kama muwekezaji wa ndani.

Kadhalika, rais mstaafu Jakaya Kikwete alikishukuru kituo hicho kwa mchango wake mkubwa katika kuleta ushindi wa CCM.

Baadhi ya vituo vingine vilivyo kwenye orodha hiyo ni pamoja na Sibuka FM, Kili FM ya Mosho, Breeze FM, Country Fm Radio, Generation Fm Radio, Hot Fm Radio Impact Fm, Iringa Municipal TV, Sumbawanga Municipal TV, Top Radio Fm, Kitulo Fm, Mbeya City Municipal TV na Ulanga Fm.

Vituo vingine ni radio Huruma, Radio Sengerema, Rock Fm, Standard Fm, Musa Television Network, Radio Pride.

 

 

Serikali yanasa wawekezaji wa madini wakiiba umeme
Celine Dion aondokewa na kaka yake, siku mbili baada ya kumpoteza mumewe