Polisi nchini Uganda imesema mtu mmoja ameuwawa na wengine 7 kujeruhiwa katika mlipuko mkubwa katika mji mkuu Kampala.

Tukio hilo ambalo Rais Yoweri Museveni amelitaja kuwa la kigaidi, limeripotiwa kutokea majira ya saa tatu usiku wa kuamkia leo katika mgahawa maarufu ulioko mtaa wa Kawempe kaskazini mwa Kampala.

Msemaji wa Polisi Fred Enanga kupitia taarifa aliyoiandika kwenye mtandao wa Twitter, amethibitisha tukio hilo na kusema majeruhi wamepelekwa katika hospitali ya rufaa ya Mulago wakiwa na majeraha mabaya.

Rais Yoweri Museveni ametaja tukio hilo kuwa la kigaidi na kuahidi kuwasaka wahusika.

Rais Yoweri Museveni wa Uganda ambaye pia ni amiri jeshi mkuu amesema watawashughulikia magaidi wote wanaojaribu kuishambulia Uganda.

Katika taarifa iliyotolewa na Rais Museveni kwenye mtandao wake amesema amefahamishwa na vikosi vya usalama kuwa watu 3 walikwenda kwenye bar hiyo na kuacha mfuko wa plastiki chini ya meza waliokuwa wamekaa, na baadaye kulipuka na kuua mtu mmoja na wengine watano kujeruhiwa.

Polisi hata hivyo imewataka raia kuwa watulivu hadi chanzo cha mlipuko huo kitakapobainika.

Ndalichako atoa maagizo Wizarani
Mfanyabiashara Mkubwa wa dawa za kulevya akamatwa Colombia