Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu amesema kuwa hakuna mtanzania yeyote aliyehisiwa au kuthibitika kuwa na virusi vya ugonjwa hatari wa Ebola, japo Tanzania iko katika hatari ya kuambukizwa ugonjwa huo kutokana na mwingiliano wa watu.

“Lakini hadi sasa hakuna mtu ambaye anahisiwa au kuthibitika kuwa na virusi vya Ebola, kutokana na kupakana na DRC, nataka kukiri kwamba tuko hatarini kuambukizwa ugonjwa huu kutokana na mwingiliano wa watu hawa wanaosafiri kutoka na kuingia Tanzania.” Ummy.

Aidha ametaka watanzania kuchukua tahadhari hususani wale wanaotumia njia zisizo rasmi kwa kuvuka Ziwa Tanganyika na mitumbwi.

Ummy ametoa tahadhari kwa nchi nzima hasa katika mikoa ambayo inapakana na DRC, ni mikoa ya Kigoma, Kagera, Mwanza, Katavi, Rukwa na Songwe ili kujikinga na ugonjwa wa Ebola, Wizara imeimarisha mfumo wa ufuatiliaji wa magonjwa ya mlipuko katika mikoa ambayo inapakana na DRC, mipakani na viwanja vya ndege vyote nchini kwa kuweka vifaa vya kubaini joto la mtu (Themo scanner).

Waziri Ummy amesema kuwa Wizara imeimarisha mfumo wa ufuatiliaji wagonjwa katika mikoa yote, kusambaza miongozo, vifaa na imeagiza makatibu tawala wa mikoa na wakuu wa mikoa kushiriki katika kutoa taarifa inapotokea dalili zozote.

“Niwatake Waganga Wakuu wa mikoa wote lakini hasa hawa ambao wanapakana DRC wasilale, wahakikishe kunakuwa na ufuatiliaji kwa wageni kwa kuweka daftari, mifumo na vifaa maalumu vya kutambua,” amesema Ummy

Aidha amesema hivi sasa kuna wodi ambayo imetengwa kwa ajili ya wagonjwa wa Ebola, watakaobainika katika Hospitali ya Rufaa ya Temeke.

Tanesco yatangaza umeme kukatika Dar
Sam Allardyce ambwatukia bosi wa DC United