Uamuzi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli, kununua korosho za wakulima na kuzibangua nchini umepongezwa na Umoja wa Wabanguaji Wadogo wa Korosho Tanzania (UWWKT).

Pongezi hizo zimetolewa na Mwenyekiti wa umoja huo, Tumpale Magehema ambapo amesema kuwa uamuzi wa Rais Magufuli una nia ya kuwapa ajira wanachama wake wapatao 2881, jambo ambalo ni la kupongezwa.

Amesema kuwa uamuzi huo wa kijasiri uliofanywa na Rais Magufuli utaongeza ari ya kufanya kazi na kuchochea ukuaji wa uchumi hasa kwenye mikoa inayolima korosho kwa wingi.

Kwa upade wake Katibu wa umoja huo, Audax Mkongi, amesema kuwa umoja huo ni asasi mwamvuli ya kitaifa ya wabanguaji wadogo yenye jumla ya vikundi 183 kutoka wilaya tisa za mikoa ya Mtwara, Lindi, Pwani na Morogoro. baadhi ya wilaya hizo ni Ulanga, Tandahimba, Kisarawe, Liwale na Ruangwa.

Aidha, naye mgeni rasmi kwenye hafla hiyo iliyofanyika mkoani Lindi, Naibu Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Stella Manyanya ameupongeza umoja huo kwa ari na nia ya kuunga mkono juhudi za serikali ya awamu ya tano ya uchumi wa viwanda.

Manyanya pia amewahakikishia ushirikiano kutoka wizara yake na kwa kuanza serikali inaandaa utaratibu wa kuutumia ili kuingia nao mikataba ya kubangua korosho iliyonunuliwa na serikali msimu huu.

Wakati huo huo, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Maendeleo ya Viwanda Vidogo (SIDO), Profesa Sylvester Mpanduji amesema kuwa taasisi yake itaendelea kushirikiana na Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Naliendele pamoja na wadau wengine wa korosho kutoa mafunzo kwa wajasiriamali wadogo na wa kati ili kuongeza thamani na ubora wa zao hilo ambalo linaongoza kwa kuliingizia taifa fedha za kigeni.

Kigogo wa CCM ashinda kesi ya rushwa
Binti wa miaka 7 amburuza polisi baba yake mzazi