Unakumbuka wiki ya kwanza ulipoianza kazi unayoifanya? Unakumbuka ulipoipata kazi hiyo uliwaambia watu wangapi na namna ulivyokuwa na furaha? Ilikuwa sherehe moyoni mwako. Kila kitu kilikuwa vizuri, ilikuwa habari njema na baraka kubwa kwako.

Mapokezi uliyopewa na muajiri wako mpya muda mfupi baada ya kusaini mkataba wako na maneno ya faraja yalikufanya ujione umeingia kwenye njia ya mafanikio haswa. Naipata picha nzima ya siku ulipokuwa unatambulishwa kwa kila mwajiri uliyemkuta ofisini.

Welcome

Huenda Boss wako alikuwa mtu mwema sana, alikukaribisha vizuri na kuanza kukuelekeza kazi na hata ulipokosea alikuwa muungwana sana kwako na kukuelekeza taratibu hadi alipohakikisha umeelewa kweli.

Lakini sasa kila kitu kimebadilika, unaichukia kwa nguvu zote ile ofisi… Boss wako anakuandama kila wakati, kila unachofanya kwake hakifai. Muda mwingine anatumia maneno makali yanayokukwaza. Kile kipato ulichokifurahia wakati unaanza kazi sasa hakitoshi kabisa. Hii inakufanya uzidishe chuki yako na unatamani uondoke punde tu ukipata pa kukimbilia.

Unahesabu saa za kazi, sasa unaziona nyingi. Unatamani muda ufike ukimbie kutoka ofisini ukapumzike kwa sababu ni chanzo kikubwa cha msongo wa mawazo ulionayo.

Sio bure, kuna uchawi katika kazi unayofanya. Ndio, uchawi unaoufahamu ila hujatambua chanzo chake.

Ngoja nikuelekeze alipo mchawi wa kazi yako:

Watu wengi wanapokuwa kwenye matatizo kama haya ofisini, huanza kufikiria mbali sana. Kila aina ya sababu itatafutwa ikiwa ni pamoja na ushirikina. Lakini kufanya hivyo ni sawa na kwenda kwa jirani kumtafuta kunguni anayekung’ata kitandani kwako. Kunguni huyo yuko ndani mwako, utapoteza muda kumsaka kwa jirani.

Jipime kama una dalili hizi:

    1. Majigambo

Katika hali ya kawaida inawezekana kweli wewe ndiye unayefanya kazi kwa bidii na unajua vitu vingi kuliko wenzako, sasa zaidi hata ya wale uliowakuta kazini. Kwakuwa unafahamu hilo, ullianza kujigamba bila taratibu. Ulitaka wote wafahamu kuwa wewe ndiye kiungo muhimu katika ofisi hiyo na hata Boss wako anakutegemea zaidi wewe.

 2. Kutangaza umeichoka kazi yako/huipendi

Unapokuwa ofisini, kuna wakati unaona wafanyakazi wenzako kama wote ni rafiki zako hususan pale mnapokuwa mnapiga polojo mida ya ‘lunch’, na ndipo unapojikuta unatoa lawama kwa Watawala au muajiri. Kueleza kuwa huipendi tena kazi hiyo. Habari hizi hufika mbali na muajiri huanza kukuona kama kikwazo kwenye timu yake.

  3. Kujihusisha na umbea

Umbea una tabia mbili. Unapojihusisha na umbea, tambua kuwa yule mnaemsema leo hatasemwa tena kesho. Habari zako zitasemwa na uliyoyasema yataripotiwa. Huenda ulikuwa unaonekana mkamilifu ulipokuwa unaingia, lakini habari anazopata Boss wako ambazo ni mazao ya umbea mliopiga kwenye ‘kolido za ofisi’, zimembadili.

Umbea

 4. Uko ‘emotional’ na unaonesha

Unapotofautiana na Boss wako, unaonesha hisia zako kwa kiwango cha juu. Kulia, kukasirika hadi kushindwa kufanya kazi za siku huku ukigonga baadhi ya vitu kuonesha hasira yako. Kuongea kwa hasira mbele ya wafanyakazi wenzako kuhusu Boss alivyokukwaza na hata kumwabia. Kugoma kula au kugoma kupokea simu za ofisini kwa sababu umekasirishwa sana. Hili ni tatizo kubwa kwenye ajira yako.

  5. Unadanganya

Wewe uligeuka kuwa bingwa wa kumpanga Boss wako, unajua nini ukimpiga ‘fix’ ataelewa. Bahati mbaya, Boss wako aliwahi kuwa kwenye nafasi yako kwahiyo anajua. Kubaini kuwa unamdanganya kunamuondolea uaminifu aliokuwa nao juu yako.

 6. Muda unaougusa mlango wa ofisi

Unaingia kazini umechelewa angalau dakika 15 na zaidi. Of Course kama uko Dar es Salaam unakuwa na jibu lako umelitenga kabisa, “Boss samahani nilikwama kwenye foleni.” Boss wako akikupigia simu ya ofisini angalau dakika 5 tu baada ya muda wa kazi hakupati kwa sababu ulishaondoka kwa kuwa ulianza kufungasha vyako dakika 15 zilizopita. Unawahi Foleni.

  7. Unajua sana

Baada ya kufanya kazi kwa muda fulani, sasa wewe ndiye mtaalam unaefahamu zaidi na kweli una akili nyingi sana. Unamuonesha Boss wako kiwango chako cha kujua na kukosoa. Kumbuka Kikombe kilichojaa maji hakiongezwi maji..!

 8. Unafanya kazi kwa bidii, kama jana kama mwaka jana (Haukui)

Unaamini unafanya kazi kwa bidii. Kama jana, kama mwaka jana. Na ukijipima na wenzako unaona unafanya kazi kama wao tu lakini unaandamwa wewe. Unapaswa kutambua kuwa haukui, hauna ubunifu na hauongezi uzalishaji. Kwa ufupi biddi yako imedumaa. Unafanya kama jana, kama mwaka jana kwa bidii. Kila mwajiri anahitaji zaidi ya bidii.. anahitaji mtu anayekua.

 9. Unabeba Kazi na Sifa za Timu kuwa zako

Unaweza kuwa unajiweka wewe kwenye kazi ambazo hukufanya peke yako na kutaka ionekane kama wewe ndiye uliyefanya zaidi. Kweli, inawezekana kuwa ulifanya wewe zaidi. Kiongozi mzuri ataona wewe unataka kuua vipaji vya wengine na kutaka usifiwe wewe kwanza.

10. Umepoteza uwezo wa kusikiliza

Kwa sababu unaamini unafahamu vitu vingi, umepoteza uwezo wa kusikiliza maelekezo kama awali. Hivi sasa wewe una uwezo mkubwa zadi wa kueleza. Unaamini unajua mengi na unataka usikilizwe wewe. Wenye uwezo wa kusikiliza zaidi ya kuzumgumza huongeza zaidi ufahamu.

Kusikiliza

Kama dalili hizi zinakuhusu… naamini tayari umeshamjua mchawi wako kazini. Mchawi wako kazini ni ‘Wewe’. Hivyo, unapaswa kubadilika haraka sana kuinusuru ajira yako iwe ya furaha.

Mramba aishauri serikali kuhusu namna ya kuwatumia wafungwa kama yeye
Miyeyusho Na Nassibu Ramadhani Wasaini Mkataba Wa Kupanda Ulingoni