Leo tunalifunga kundi F tukikamilisha kuimulika Korea Kusini baada ya kumulika timu nyingine kwenye kundi hili ambazo ni Ujerumani, Mexico na Sweden.

Ilikua safari ndefu kwa nchi ya Korea Kusini iliyofuzu kucheza fainali za kombe la dunia ikitokea ukanda wa barani Asia.

Ilianza kushiriki harakati za kuwania kufuzu fainali hizo kuanzia mzunguuko wa pili uliohusisha makundi manane ya ukanda wa Asia. Korea Kusini ilipangwa katika kundi la saba lililokuwa na timu za Lebanon, Kuwait, Myanmar na Laos.

Katika michezo ya mzunguko wa pili kupitia kundi hilo, Korea Kusini ilifanikiwa kupita na kuingia kwenye mzunguuko wa tatu, baada ya kuongoza msimamo wa kundi hilo kwa kupata alama 24.

Mzunguuko uliofuata Korea Kusini ilipangwa katika kundi la kwanza lililokuwa na timu za Iran, Syria, Uzbekistan, China na Qatar.

Taifa hilo la mashariki ya mbali lenye watu zaidi ya 51,446,201, lilimaliza katika nafasi ya pili kwenye msimamo wa kundi hilo ikitanguliwa na Iran, na kufanikiwa kufuzu moja kwa moja katika fainali za kombe la dunia za mwaka huu 2018.

Majina ya utani ya timu ya taifa ya Korea Kusini: Taegeuk Jeonsa, “Taegeuk Warriors”) The Reds au Red Devils, Asian Tigers na Taegeuk Tigers

Mfumo: Kikosi cha Korea Kusini hutumia mfumo wa 4-4-2.

Image result for Son Heung-min - south koreaMchezaji Nyota: Son Heung-min (Tottenham Hotspur)

Image result for Kwon Chang-hoon - south koreaMchezaji hatari: Kwon Chang-hoon (Dijon)

Image result for Ki Sung-yueng - south koreaNahodha: Ki Sung-yueng (Swansea City).

Image result for Shin Tae-Yong  - south koreaKocha: Shin Tae-Yong (49), raia wa Korea Kusini.

Ushiriki: Korea Kusini imeshiriki fainali za kombe la dunia mara tisa (9). Mwaka 1954, 1986, 1990, 1994, 1998, 2002, 2006, 2010 na 2014.

Mafanikio: Mshindi wa nne (2002).

 

Kuelekea 2018:

Timu ya taifa ya Korea Kusini imekuwa inaonyesha jitihada za kufika mbali na ikiwezekana kutwaa ubingwa wa dunia, mara zote walizoshiriki timu hii huonekana kuwa tayari kupambana na yoyote.

Hatua hiyo ya kujiamini kwa kikosi hicho imeanza kutoa matumaini ya kuongeza chachu ya ushindani wakati wa fainali za kombe la dunia za mwaka huu.

Timu hiyo hupenda kucheza soka la kushambulia mara kwa mara, na ni mara chache sana kuonesha mchezo wa kuzuia.

Kocha Shin Tae-yong ambaye aliwahi kuwa kocha wa timu ya taifa chini ya umri wa miaka 23 ya taifa hilo, hana sifa kubwa ya ufundi anapokuwa katika majukumu yake, lakini anapambwa na sifa ya kuwa mhamasishaji kwa wachezaji wake ndani ya dakika 90.

Mashabiki wa soka Korea Kusini wanamuamini sana kocha huyo na wanatarajia kuona akifanya kazi yake ya kuhamasisha wakati wote pindi kikosi chao kitakapokuwa na jukumu la kupambana nchini Urusi.

Korea Kusini wataanza kampeni za kuusaka ubingwa wa mwaka huu kwa kucheza dhidi ya Sweden, Uwanja wa Nizhny Novgorod mjini Nizhny Novgorod Juni 17, kisha watapambana na Mexico Juni 23, Uwanja wa Rostov mjini Rostov-on-Don, na mchezo wao wa mwisho hatua ya makundi watakutana na mabingwa watetezi Ujerumani Juni 27, Uwanja Kazan mjini Kazan.

Taifa hili ambalo lipo kwenye vichwa vya habari karibu kila siku kuhusu mgogoro wa kinyuklia wa Rasi ya Korea limepania kuandika historia nyingine kwenye vichwa vya habari vya michezo. Je, watafanikisha, tusubiri majibu wiki chache zijazo.

Sisi jukumu letu ni kuendelea kukujuza kuhusu timu uzipendazo, endelea kuwa nasi. Kesho tutaanza kulimulika kundi G. Usiache kufuatilia pia channel yetu ya YouTube ya Dar24 Media.

Juventus wamchukua jumla Douglas Costa
Frederico Rodrigues de Paula Santos “Fred” azua hofu kambi ya Brazil