Urusi inajipanga kuzima Mtandao wa Intaneti kwa muda, na hivyo kujitoa kwenye mawasiliano na dunia kama sehemu ya majaribio yake ya kujikinga dhidi ya mashambulio ya kimtandao.

Zoezi hilo litafanya mawasiliano baina ya raia na mashirika ya Urusi kubaki ndani ya nchi badala ya kupitia njia za kawaida za kimtandao kimataifa.

Rasimu ya sheria ya kuruhusu mabadiliko ya kiufundi ili kuiwezesha nchi hiyo kuendesha mtandao wake wenyewe iliwasilishwa bungeni na kupewa jina la Programu ya Taifa ya Uchumi wa Kidijiti, ambayo inawataka watoa huduma za intaneti nchini Urusi kuwa na uwezo wa kuendelea na huduma zao hata pale ikitokea nchi za kigeni zikiamua kuitenga Urusi.

Nchi wanachama wa NATO na washirika wake wamekuwa wakitishia kuiwekea vikwazo vya kimtandao Urusi ambayo wanaituhumu kwa kufanya mashambulio mengi zaidi ya kimtandao.

Aidha, njia mojawapo inayopangwa na Urusi katika kujilinda huko ni kutengeneza mfumo wake binafsi wa anuani za kimtandao ufahamikao kama DNS, utakao wezesha kupata mawasiliano hata pale watakapotengwa ama kujitenga.

Hata hivyo tayari kuna chapa nyingi za mfumo huo wa DNS nchini Urusi hali inayoonesha kuwa nchi hiyo inaweza kuendelea na shughuli zake za kimtandao hata ikitokea imetengwa leo.

Watoa huduma za intaneti wanatarajiwa kuelekeza mawasiliano yote yanayopita kwao kwenye vituo vya serikali kwenye zoezi hilo, mawasiliano yote ya ndani ya Urusi yataruhusiwa kuendelea lakini yale yatokayo nje ya nchi yataminywa.

Hospitali yakanusha kuhusika kifo cha aliyefia hospitalini kwao
Prof. Mbarawa azitaka mamlaka za maji kujitegemea