Kamishna Mkuu wa Skauti Tanzania, Mwantumu Mahiza ameshtushwa na taarifa za kuwepo kwa baadhi ya wanafunzi wa shule za mkoani Tanga wanaojihusisha na mapenzi ya jinsia moja, na kutoa kauli ya kukemea.

Akizungumza hivi karibuni akiwa mkoani humo, Mahiza ambaye pia amewahi kuwa Naibu Waziri wa Elimu amesema taarifa hiyo imemshtua kwani mbali na kuwa kinyume na maadili na sheria za nchi, inawadidimiza kitaaluma wanafunzi na Taifa.

Alieleza kuwa taarifa ya kuwepo kwa vitendo vya ushoga na usagaji pamoja na mahusiano ya mapenzi shuleni, ilitolewa na Mkuu wa Wilaya ya Pangani, Zainab Abdallah alipotembelea shule ya Sekondari Funguni akiwa na Naibu Katibu wa Umoja wa Wanawake wa CCM (UWT) Taifa, Jesca Mbogo aliyekuwa ziarani mkoani humo.

Akimkariri Mkuu huyo wa Wilaya, Mahiza alisema, “vijana wengi wanajihusisha na mahusiano ya mapenzi shuleni, kuna wachumba, wasagaji, na watumiaji dawa za kulevya. Lakini zipo jitihada tumeanza kufanya kupambana na suala hilo,” alisema Mahiza.

Aliongeza kuwa kutokana na hali hiyo, Serikali inapaswa kuwatuma wataalam husika haraka ili kuchunguza vitendo hivyo na kuvikomesha.

Naye Mwenyekiti wa Wilaya ya Pangani wa CCM, Hamisi Mnegero amekiri kufahamu uwepo wa vitendo hivyo mashuleni na kueleza kuwa havipaswi kufumbiwa macho.

Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Martin Shigella ameahidi kuzifanyia kazi haraka iwezekanavyo taarifa hiyo hatari kwa ustawi wa Taifa lenye maadili mema.

Mkoa wa Tanga umekuwa kwenye mfululizo wa orodha ya mikoa kumi inayofanya vibaya katika matokeo ya kidato cha nne.

Mwaka huu, katika matokeo ya kidato cha nne, kati ya shule kumi za mwisho, tatu zimetoka mkoani Tanga ambazo ni Kwediboma, Komkalakala, Seuta.

Mkoa huo una historia mbaya ya matokeo hayo kwa miaka mitatu mfululizo, mwaka 2016 ulikuwa wa tatu kutoka mwisho, na 2017 ulikuwa mkoa wa 24 kati ya mikoa 30.

Familia yapoteza watoto watano kwa kula samaki wenye Sumu
Joti amlilia Mama Abdul, 'mwanao sina cha kuongea'