Waziri wa Madini, Angela Kairuki amesema kuwa uwekezaji katika sekta ya madini umeongezeka, hasa kwa wawekezaji wa nje kutoka katika kipindi cha miaka miwili iliyopita tangu sheria ya madini ya mwaka 2010 ifanyiwe marekebisho na kuanza kutumika mwaka 2017.

Akizungumza mara baada ya kongamano la uwekezaji katika sekta ya madini kati ya Tanzania na China lililofanyika Beijing nchini China Jumatatu wiki hii, Kairuki alisema kasi ya uwekezaji katika sekta ya madini imeendelea kuongezeka baada ya kufanya marekebisho hayo ya sheria na hivyo kuboresha mazingira ya uwekezaji kwa ujumla,..

“Wizara yangu inafanya kila liwezekanalo katika kuvutia uwekezaji wa sekta ya madini,  kwa sasa tunalo ongezeko kubwa kwenye uwekezaji huo na hii inatokana na marekebisho ya baadhi ya sheria ambazo zilipitwa na wakati,” amesema Kairuki.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania, Geoffrey Mwambe amesema kuwa Serikali imeendelea kuweka mazingira mazuri kwa wawekezaji wa ndani na nje ya nchi, na akaeleza kwamba ofisi yake haijapokea ombi lolote la mwekezaji kutaka kufuta uwekezaji wake nchini kama inavyodaiwa na vyombo vya habari vya Magharibi.

Akizungumza kwa niaba ya wawekezaji kutoka China, Mwenyekiti wa Kampuni ya SunShine iliyowekeza katika sekta mbalimbali nchini, Tony Sun amesema kuwa ameridhishwa na mapinduzi makubwa yanayofanywa na Serikali kwa sasa kwenye sekta ya madini, ambayo yamelenga kunufaisha wawekezaji pamoja na watanzania kwa ujumla.

Kongamano la Uwekezaji katika sekta ya madini ambalo limeandaliwa na Wizara ya Madini Tanzania kwa ushirikiano na Kituo cha Uwekezaji nchini, pamoja na Ubalozi wa Tanzania nchini China, umekutanisha watendaji wa serikali na sekta binafsi kutoka China na Tanzania. Ujumbe wa China umeongozwa na Naibu Waziri wa Maliasili, Ling Yueming, kushirikiana na Kituo.

Mtanzania ashinda tuzo za ubunifu wa teknologia Duniani
Rais wa zamani apigwa marufuku kukanyaga Marekani