Baraza la wadhamini wa klabu ya Simba linaloongozwa na Khamis Kilomoni limesema kuwa haliutambui mkutano mkuu wa klabu hiyo unaotarajiwa kufanyika mapema mwezi ujao.

Akiongea mbele ya waandishi wa Habari, katibu wa baraza la wadhamini hao, Fikilini Mkwabi amesema kuwa wao hawautambui mkutano huo kwani viongozi ambao wameandaa mkutano hawana mamlaka ya kuchukua jukumu hilo la kuitisha mkutano mkuu.

Amesema kuwa kipindi hiki si kipindi cha kujadili hoja ya mabadiliko wakati viongozi wakuu wa klabu waliochaguliwa na wanachama wanatuhumiwa na vyombo vya sheria hivyo  amewaasa kuelekeza nguvu katika kuwasaidia viongozi hao.

Naye mwanachama mkongwe wa chama hicho, Chuma Suleiman maarufu kwa jina la Bi Hindu amesema kuwa viongozi wanaokaimu nafasi hizo hawana uwezo wa kuandaa mkutano huo, hivyo kama wana mapenzi na Klabu hiyo basi wafanye jitihada za kuwasaidia walioko jela.

Hata hivyo, mmoja wa wanachama hao aliyejitambulisha kwa jina la Said Bedui amesema kuwa  kwa upande wao wamebaini kuwa mkutano huo una lengo la kufanya mabadiliko ya katiba ili klabu hiyo iwe katika mfumo wa hisa ambapo kwao jambo hilo hawalitaki kwa kuwa wanachama hawana elimu ya kutosha juu ya mfumo huo.

Nisha awaponda wanaume kama mabinti
Mabawa aja na kampeni ''Magufuli Baki'' nchi nzima