Kampuni ya DataVision International iliyoko jijini Dar es Salaam inayotoa huduma za Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (Tehama), leo imesherehekea miaka 20 ya kutoa huduma bora na kusadia jamii.

Kampuni hiyo iliyoanzishwa mwaka 1998, imeeleza namna ambavyo imefanikiwa kutoa huduma bora huku ikitoa misaada kwa jamii kwa lengo la kuokoa maisha, kutunza mazingira, kulea na kukuza vipaji, kuhuisha ukuaji wa kipato kwa wabunifu nchini na kutoa ajira kwa maelfu.

Akizungumza katika makala maalum, Mkurugenzi wa Masoko na Mahusiano wa kampuni hiyo, Bi. Teddy Qirtu amesema kuwa kampuni hiyo katika kipindi chote cha miaka 20 iliwekeza katika kuhuisha maisha na teknolojia kwa maendeleo endelevu.

Alisema kuwa hatua hizo zimekuwa zikichukuliwa kila mwaka kama sehemu ya kurejesha kwa jamii inayoizunguka.

Akitoa mfano wa jinsi ambavyo kampuni hiyo ilishiriki katika jitihada za kuokoa maisha ya Watanzania, Bi. Qirtu amesema kuwa kampuni hiyo kwa kushirikiana na wadau wake, kupitia kampeni ya ‘Tuko Pamoja’, mwaka jana ilifanikiwa kugharamia matibabu nchini India kwa ajili ya mwanafunzi wa kike wa sekondari, Mariam aliyekuwa amefanyiwa upasuaji wa tumbo mara kumi hapa nchini bila mafanikio.

“Mariam alikuwa anasumbuliwa na tatizo la utumbo kujifunga (Intestinal Obstruction). Baada ya kufahamu anachopitia na kuwa alishafanyiwa oparesheni kumi hapa nchini, tulishirikiana na wadau wetu na tuliweza kuchanga na kumpeleka Mariamu nchini India kwa ajili ya matibabu [zaidi] na akarudi akiwa na hali nzuri,” alisema Bi. Qirtu.

Mbali na hatua hiyo, alikumbuka pia namna ambavyo kampuni hiyo ilitoa msaada kwa watoto wanaotibiwa saratani kwenye kituo cha Matumaini kilichoko katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili.

Aidha, alieleza kuwa kampuni hiyo inasherehekea miaka 20 kwa kujivunia pia jinsi ambavyo iliweza kuwajali watoto wanaoishi katika mazingira magumu, ikiwa ni pamoja na kituo cha Kimbagulilo Children Centre kilichoko jijini humo.

Akizungumzia jinsi ambavyo kampuni hiyo imeshiriki kuboresha sekta ya sanaa nchini kwa kutumia teknolojia, alisema kuwa kupitia Mradi wa Utambuzi wa Wasanii wa Sanaa za Ufundi (TACIP), wamewezesha kusajili wasanii wa sanaa za ufundi nchini pamoja na kuwaongezea wigo wa kuuza kazi zao kwenye soko la kimataifa.

Katika hatua nyingine, Kampuni hiyo imeeleza kuwa imeendelea kuungana na juhudi za Serikali za kumuinua msichana na kumhamasisha kupenda michepuo ya sayansi ili kuongeza wataalam katika sekta hiyo.

“Tutakuwa na program inaitwa ‘girl coder’ ambayo inamsaidia mtoto wa kike kuanzia umri mdogo kabisa aweze kujua namna ya kutengeneza mifumo ya Tehama itakayomuwezesha yeye na jamii aliyonayo kurahisisha shughuli mbalimbali,” Bi. Qirtu anakaririwa.

Afisa Mtendaji Mkuu na mwanzilishi wa kampuni hiyo, Geofrey Mwaijonga amewahi kueleza kuwa kampuni hiyo imetoa ajira kwa maelfu ya watanzania huku ikiwanoa vijana ambao wameweza kufanya kazi na makampuni mengi ya kitaifa na kimataifa.

Tunawapongeza kwa kutimiza miaka 20 ya kazi nzuri na mafanikio yaliyojikita katika kuinua hali ya jamii. #Happy20Anniversary

Bahari hatarini kuwa na plastiki zaidi ya samaki, makampuni yajipanga
Video: Chanzo kifo cha Isaack Gamba chatajwa