Timu ya taifa ya England maarufu kama ‘Simba watatu’, imetinga hatua ya robo fainali baada ya kuibuka na ushindi wa jumla ya penati 4-3 baada ya dakika 120 kuisha kwa sare ya 1-1 dhidi ya Colombia kwenye mchezo wa 16 bora uliomalizika.

England ambayo iliongoza kwa bao 1-0 kutoka dakika ya 57 ilijikuta kwenye wakati mgumu baada ya kusawazishiwa bao hilo katika dakika ya 90, hivyo kulazimu mchezo kwenda katika dakika za nyongeza kabla ya penati kuamua.

Katika mchezo huo mshambuliaji na nahodha wa England Harry Kane alifunga bao la England hivyo kufikisha mabao 6 na kuifikia idadi sawa ya mabao kama aliyofunga James Rodriguez wa Colombia kwenye fainali za mwaka 2014 nchini Brazil ambapo aliibuka mfungaji bora.

Aidha, Jordan Pickford amekuwa golikipa wa kwanza wa England kupangua penati kwenye mechi ya mashindano tangu alipofanya hivyo kipa wa zamani wa England David Seaman dhidi ya Argentina mwaka 1998.

Hata hivyo, Penati za England zimefungwa na Harry Kane, Marcus Rashford, Kieran Trippier na Eric Dier huku Jordan Henderson akikosa. Kwa upande wa Colombia waliofunga ni Radamel Falcao, Juan Cuadrado na Luis Muriel huku Mateus Uribe na Carlos Bacca wakikosa. England sasa itakutana na Sweden kwenye mechi ya robo fainali siku ya Jumamosi.

Sudan Kusini kurefusha kipindi cha utawala wa rais Salva Kiir
Habari kubwa katika Magazeti ya Tanzania leo Julai 4, 2018