Mgombea urais kwa tiketi ya Chadema, Edward Lowassa jana alifanya mahojiano maalum na BBC kupitia kipindi cha Dira ya Dunia na kujibu maswali mbalimbali.

Pamoja na mambo mengine, Lowassa alizungumzia jinsi atakavyowezesha elimu bure hadi chuo kikuu, kuhusu afya yake pamoja na mabadiliko anayaoyahuribi.

Hivi ndivyo ilivyokuwa:

Edward Lowassa: Watanzania wengi sana hawapati elimu, hawapati elimu inayopasa, elimu bora. Unajua dunia ya sasa imebadilika. Dunia ni Teknolojia. Ajira za dunia huzipati kama huna elimu inayopasa. Na sisi elimu tunayotoa kwa kweli hatuwezi ku-compete katika dunia ya leo.

Zuhura Yunus: Lakini Mhe. Suala ni hilo la bure. Kwa sababu tayari tunajua walimu wamekuwa wakilalamika sana mishahara yenyewe ni midogo. Hizo fedha zitatoka wapi, za mpaka watu waende bure?!

Edward Lowassa: Mbona wanazoendeshea mashangingi zinatoka wapi? Kuna mashangingi makubwa sana ya Milioni 230 mtu mmoja. Utakosa hela za kugawa kwa ajili ya wanafunzi? Au kwa mfano, pesa za gesi, tuna gesi nyingi tu kutoka kusini sasa hivi.

Zuhura Yunus: Kwahiyo nahisi tukitegemea gesi kwa sasa haitokuwa sawa. Kuna namna nyingine?

Edward Lowassa: Kwanza kwamba gesi haitokuwa sawa si kweli. Ghana walikuwa na mgogoro kama hivi hivi. Lakini wakaruhusiwa kukopa Gas Reserve. Unakopa Gas Reserve kwamba itakapofika mwaka fulani nita…..kiasi fulani, nitawalipeni kodi lenu. Ingawa wanasema mpaka 2020, tunaweza kuanza kutumia kwa kukopa…. … kuwekeza katika miundo mbinu na rasilimali zinazostahili.

Zuhura Yunus: Kitu gani kimefanya mpaka sasa hivi isiwezekane (elimu) kuwa bure? Maana’ke unasema inawezekana lakini kwanini mpk sasa?

Edward Lowassa: Waulize walionitangulia.

Zuhura Yunus: Mheshimiwa, wewe umekuwa, tukizungumzia suala hilo la waliokutangulia, umekuwa katika chama cha CCM kwa takribani miaka 35, kwahiyo ulikuwa katika serikali hiyo, bila shaka ulikuwa na uwezo wa kutekeleza hayo ya elimu bure, lakini…..

Edward Lowassa: Ukitaka kutekeleza ni yule mwenye mamlaka. Ama ni waziri, ama ni waziri mkuu ama ni rais. Lakini vilevile, nilipokuwa waziri mkuu nimesimamia elimu. Tulijenga shule za sekondari kwenye kila kata ya nchi hii.

Zuhura Yunus: Hilo ni jambo jema wote kupata elimu lakini si ya bure. Na ambapo ulikuwa katika nafasi ya Uwaziri Mkuu ambayo ulikuwa na uwezo wa kupendekeza hilo la elimu bure..

Edward Lowassa: Mimi sioni kwanini unaugua habari ya bure! Inawezekana. Hivi huko Ulaya wanatoza shule kodi?

Zuhura Yunus: Sikatai mheshimiwa kwamba inawezekana, lakini nani atatekeleza? Kwa sababu kila mtu anaahidi, kila mtu anasema, lakini watekelezaji..

Edward Lowassa: Watanzania wanipe Mandate tarehe 25 Oktoba utaona nitakavyoitekeleza.

Zuhura Yunus: Lakini ulikuwa na nafasi hiyo zaidi.. Umechukua nafasi nyingi za uwaziri mheshimiwa, mpaka Waziri Mkuu si jambo dogo hilo..

Edward Lowassa: Nisikilize basi. Ndio maana naomba nafasi hiyo sasa. Tarehe 25 Oktoba wakinipa Mandate hiiyo utaona utekelezaji wake. Na mimi nakuahidi Wallahi itakuwa maajabu!

Zuhura Yunus: Kwahiyo unatakiwa uwe rais ndio uweze kutekeleza hayo, sio? Huwezi kuwa waziri tu, waziri mkuu, mbunge..

Edward Lowassa: Kuna mambo ambayo waziri huna mamlaka nayo.

Zuhura Yunus: Kwahiyo uliwahi kushauri suala hilo likakataliwa?

Edward Lowassa: Nina hiyari ya kukataa na kukubali.. Kusema kwamba nilishauri au sijashauri siwezi kusema!

Zuhura Yunus: Ufisadi: Una mkakati gani wa kupambana nao? Manake ufisadi huo uko katika ngazi ya juu mpk ya chini

Edward Lowassa: Hilo ni swali gumu, refu na lingetaka mjadala wake peke yake. Mimi nimetafakari, kwa kuanzia tu, tuanze na One stop center. Ambako huko huduma za serikali zinapatikana. Kwahiyo nikija, dirisha hili linapata hiki, dirisha hili linapata kile, nikiondoka nimemaliza kazi. Tupunguze kidogo urasimu.

Zuhura Yunus: Na katika ngazi ya juu? Hizo ni katika ngazi za chini lakini kuna viongozi…

Edward Lowassa: Ngazi ya juu ningetaka kulitafakari kidogo. Wametoa taarifa juzi ya PPA ya hali ya Ufisadi ulivyo nchini na kuorodhesha wizara zile ambazo zinaongoza.

Zuhurua Yunus: Unajinadi Mabadiliko. Ni mabadiliko gani hasa?

Edward Lowassa: Baada ya miaka 50 ya kujitawala, tunataka mabadiliko katika nchi yetu.

Zuhura Yunus: Mabadiliko hayo unahisi kwa upande wa UKAWA ndio yanaweza yakafanyika?

Edward Lowassa: Sio nahisi tu, naamini hivyo.

Zuhura Yunus: Kuna tofauti gani ambayo unahisi kule ulishindwa kufanya utaweza kufanya wakati ukiwa UKAWA?

Edward Lowassa: Miaka ya nyuma kabisa Mwalimu amesema, akitambua kwamba ndani ya CCM huwezi kupata mabadiliko, nje ya CCM ndio unaweza kubadilika kwa sababu ni mfumo. Nahitaji kubadilisha mfumo mnzima.

Zuhura Yunus: Lakini Mheshimiwa ukisema sera za CCM.. Una kama Miezi kadhaa tu ulikuwa humo humo. Na bilashaka kama usingekatwa ungebaki na mfumo na sera hizo hizo za CCM, si ndio?

Edward Lowassa: Unanionea! Mimi nimekuwa mbunge wa kawaida toka miaka 8 iliyopita, sikuwa na madaraka yoyote katika nchi, nilikuwa mjumbe wa vikao lakini sikuwa na madaraka katika nchi.

Zuhura Yunus: Baadhi ya wapinzani wanasema kutokana na nafasi hii kubwa ya urais, wamekuwa wakizungumzia afya yako. Wewe unawaambiaje?

Edward Lowassa: Afya yangu nzuri kabisa!

Zuhura Yunus: Kwa mfano, ikatokea hukufanikiwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, nini mipango yako?

Edward Lowassa: Nitakuja kuchunga Ng’ombe. Nina Ng’ombe, nitakaa na Ng’ombe wangu kijijini na kuendelea na maisha..

 

 

 

Magufuli Aonya Wanaokimbilia Mahakamani Kuzuia Miradi
Joe Biden Amuondolea Kikwazo Hillary Clinton, Urais Wa Marekani