Mjadala mkuu na muhimu leo kwenye vyombo vya habari, mitandao ya kijamii pamoja na maeneo ya mikusanyiko ni mabadiliko ya viongozi wa wilaya, mkoa na wizara yaliyofanywa na Rais John Magufuli yakitajwa majina kadhaa mapya kwenye nafasi hizo.

Kati ya majina hayo, Rais Magufuli amewapa nafasi vijana watatu wenye ushawishi mkubwa kwenye masuala ya siasa bila kufikia nafasi ya ubunge, Patrobas Katambi, mwanamitindo Jokate Mwegelo pamoja na mwandishi wa habari, Jerry Muro.

Jokate amepata nafasi hiyo ikiwa ni mara kwanza kuingia kwenye mfumo wa Serikali akiteuliwa kuwa Mkuu wa Wilaya ya Kisarawe. Awali, Jokate aliwahi kuwa Kaimu Katibu Idara ya Uhamasishaji ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) lakini alienguliwa.

 

Hata hivyo, mbali ya siasa, Jokate aliyewahi kushika nafasi ya pili kwenye mashindano ya urimbwende ya Miss Tanzania mwaka 2006, aliwahi pia kuwa mtangazaji wa TV (Channel O), muigizaji wa filamu na  mjasiriamali.

Kwa upande wa Jerry M

Jokate Mwegelo

uro ambaye alianza kushika vichwa vya habari nchini akiwa mtangazaji wa kipindi cha ‘Usiku wa Habari’ cha TBC1, akitokea ITV, jina lake lilishika kasi kwenye mitandao ya kijamii na vyombo vya habari alipokuwa msemaji wa klabu ya Yanga.

Muro aliyewahi kutaka kugombea ubunge kwenye jimbo moja jijini Dar es Salaam, hivi karibuni alikuwa mstari wa mbele kutetea maslahi ya Chama Cha Mapinduzi dhidi ya shutuma zilizokuwa zinaelekezwa kwenye chama hicho na vyama vya upinzani.

Kishindo kingine kilichosikika leo, ni uteuzi wa aliyekuwa Mwenyekiti wa Baraza la Vijana Chadema (BAVICHA), Patrobas Katambi ambaye ameteuliwa kuwa Mkuu wa Wilaya ya Dodoma.

Uamuzi wa Katambi kutoka Chadema huenda ulikuwa uamuzi sahihi kwake ambao umempa nafasi ya kuwa na sifa ya kujiunga na Serikali ya CCM. Akiwa Chadema na hata alipohamia CCM, sauti yake ilikuwa miongoni mwa sauti za vijana wachache ambao walikuwa wanasikika kwa kishindo kwenye uwanja wa siasa.

Wengine waliopata uteuzi mzito leo ni pamoja na David Kafulila maarufu kama mzee wa Escrow, aliyeteuliwa kuwa Katibu Tawala Mkoa (RAS) wa Songwe. Na kijana mwingine ni Ally Hapi ambaye alikuwa mkuu wa wilaya ya Kinondoni na sasa ni Mkuu wa Mkoa wa Iringa. Kafulila aliwahi kuwa mbunge machachari wa jimbo la Kigoma Kusini kwa tiketi ya NCCR – Mageuzi. Alihamia CCM baadaye akiwa sio mbunge. Rais Magufuli aliwahi kumsifia kabla hajahamia CCM kwa jinsi alivyoweza kuibua sakata la Escrow alipokuwa bungeni.

Amos Makalla, aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Mbeya amehamishiwa Katavi huku nafasi yake ikichukuliwa na Albert Chalamila.

Kabla ya kuteuliwa kuwa Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Chalamila alikuwa Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Iringa.
Angalia video hapa:

Agundua jinsi ya kutumia SMS kubana matumizi ya umeme
Klopp ajibu kejeli za Mourinho, amtaja kwenye malengo yake