Ushindi wa Klabu ya Simba dhidi ya JS Saoura ya Algeria, ulioongeza mwanga wa nyota ya Tanzania kwenye michuano ya Kimataifa umemkuna Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Wallace Karia na kumfanya afunguke mambo kadhaa.

Simba kupitia kwa Emmanuel Okwi na Meddie Kagere imejizolea alama tatu kwa kugawa kipigo cha 3-0 dhidi ya Tai wa Algeria, hivyo kujiweka katika nafasi nzuri ya kufanikisha kupenya hatua ya makundi.

Akizungumza na Dar24 kwenye mahojiano maalum muda mfupi baada ya mechi hiyo kumalizika katika Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, Karia amesema kuwa ushindi wa Simba ni ushindi wa Watanzania wote.

Akizungumzia hali ya mchezo, Kiongozi huyo wa TFF alieleza kuwa Simba ilipata nafasi nyingi za kupachika magoli lakini kwa bahati nzuri nafasi chache kati ya hizo zilitumika vizuri na kuleta ushindi.

Aidha, Rais huyo wa TFF aliwaasa viongozi na wachezaji wa Klabu ya Simba kuhakikisha kuwa wanaepuka migogoro ili kufanikisha azma ya kunyakua ushindi wa Kombe la Mabingwa Barani Afrika.

“Mimi niwape rai viongozi wa Simba pamoja na mashabiki wao waendelee kushirikiana na kuwa kitu kimoja ndio matokeo kama haya yanaweza kupatikana,” alisema Kiria.

Angalia video ya mahojiano hapa chini kumsikiliza akifunguka kuhusu utabiri wake kwa Simba katika michezo ijayo, akiwafunda kuhusu utatuzi wa migogoro, alivyofanikisha ushindi mara kadhaa kwenye Uwanja wa Taifa pamoja na ushabiki:

Mpinzani apinga matokeo ya Urais wa DRC Mahakamani
Waumini wamgeuka Imam msikitini, wataka aongoze maandamano