Wakala wa Majengo nchini Tanzania, taasisi ya Serikali iliyopo chini ya Wizara ya Ujenzi Uchukuzi na Mawasiliano (TBA) ambayo inatekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo katika sekta ya ujenzi nchini, mwaka huu imeandaa utaratibu maalum wa kufanya malipo ya nyumba za makazi na ofisi kwa wateja wake ambao utatumia mfumo wa kielektroniki utakaomuwezesha mteja kufaya malipo mahali popote.

TBA inayojihusisha na uuzaji pamoja na upangishaji wa nyumba kwa vongozi wa serikali na watu binafsi, imekuja na utaratibu wa aina nne ambao utamuwezesha mteja wa nyumba kuwa na uhuru wa kuchagua utaratibu rafiki wa kulipia makazi hayo.

Akizungumza na Dar24Media Mshauri Mwendelezaji Miliki kutoka TBA, Shauri Ramadhan kwenye maonyesho ya biashara ya 43 ya Kimataifa yanayofanyika katika viwanja vya Sabasaba amethibitisha kuwa utaratibu huo utamsaidia mteja kulipia kwa urahisi gharama za nyumba.

Akitaja taratibu hizo amesema mteja wa nyumba anaweza kufanya malipo kwa pesa taslimu kwa mkupuo, kulipa kwa kutumia mkopo wa benki, na kwa wastaafu kufanya malipo kwa kutumia mafao yao na utaratibu wa mwisho ni ule wa kufanya malipo ya asilimia 10 ya nyumba yote huku pesa iliyobaki ikilipwa taratibu mtu akiwa ndani ya nyumba yake kwa kipindi cha muda fulani kulingana na mkataba.

”Kwakweli kwasasa mteja wetu au mtumishi anaweza kufanya malipo kwa njia nne ambapo atakuwa na uhuru wa kuchagua atumie njia ipi ambayo ni rahisi kwake,”amesema Ramadhani

Amesema hatua hizo ni kufuatia kuondokana na changamoto mbalimbali ambazo zimekuwa zikiwakumba wateja wao ikiwemo usumbufu unaojitokeza wakati wa malipo ambao kwa kiasi kikubwa kwa kutumia mfumo wa kielektroniki itapunguza usumbufu huo.

Aidha, Ramadhani amewahamasisha wananchi na wadau mbalimbali kutembelea banda la TBA lililopo katika viwanja vya Sabasaba ili waweze kujifunza mambo mbalimbali yanayohusu Wakala wa Majengo Tanzania na kupata  maelekezo kwa kina juu ya taratibu hizo mpya za malipo.

Hadi kufikia sasa TBA imefanya miradi mbalimbali ya maendeleo hapa nchini ikiwemo ujenzi wa mabweni ya wanafunzi wa chuo kikuu cha Dar es salaam, Magufuli Hosteli zilizopo Ubungo mkabala na jengo la TCRA, Ujenzi wa shule ya Ihungo iliyopo Bukoba ambayo awali ilianguka kutokana na tetemeko la ardhi.

Bofya hapa kutazama zaidi.

 

Habari kubwa katika Magazeti ya Tanzania leo Julai 10, 2019
Fanyeni utafiti kwanza kabla hamjatoa habari nyeti- Dkt. Tulia Ackson