Watetezi wa Haki za Binadamu nchini wameungana na kuzindua operesheni maalumu ya ‘Tetea Haki za Mtuhumiwa’ nchi nzima wakianza na Mkoa wa Arusha wilayani Ngorongoro.

Watetezi hao ni Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu Tanzania (LHRC) na Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu (THRDC), ambao wamesema lengo lao ni kupambania waathirika wa matukio ya watu kukamatwa na kukaa mahabusu bila hatia.

Hayo yamesemwa jijini Dar es salaam na Mratibu wa Kitaifa THRDC, Onesmo Olengurumwa alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari, ambapo amesema kuwa licha ya kukaa wiki nzima lakini pia walifanyiwa vitendo vya kikatili jambo ambalo halifai katika taifa.

Aidha, watetezi hao wameitaka Serikali na uongozi wa juu wa Jeshi la Polisi kuwachukulia hatua kali za kisheria askari Polisi waliohusika na ukatili mbalimbali kwa baadhi ya watuhumiwa hasa waliokamatwa hivi karibu huko Loliondo ambao baadaye waliachiwa mwishoni mwa wiki.

Katika hatua nyingine Watetezi hao wamewataja wananchi waliowekwa mahabusu kwa wiki nzima kuwa ni pamoja na Peter Orkery, Musa Yahya, Kayanda Kisoki, Zakaria na Francis Arusha ambao walikamatwa na Jeshi la Polisi Wilayani Ngorongoro tangu Desemba 21, mwaka jana hadi Januari 4, mwaka huu.

 

Habari kubwa katika magazeti ya Tanzania leo Januari 23, 2019
Uwindaji panya waharibu misitu